Asalaam Aleiykum
(وَأَمَّآ إِن كَانَ مِنَ ٱلۡمُكَذِّبِينَ ٱلضَّآلِّينَ )
Ama kama ulikua katika wale walokadhibisha, ukawa kwenye udhalimu, basi leo hasara ilioje, waliokuzunguka kitandani wanaona uko salama, kumbe ndani una jungu la maji ya moto kidogo kidogo umepewa ulimalize ndio Roho itoke, Kama itatokea uachwe peke yako japo kwa muda kidogo watu waende nje kwa mapumziko, wakirudi wanaweza kurejea wakakukuta ushameza shuka ya kulalia yote.
Utatamani wakati huo itolewe (Pipe) ikatiwe baharini ili upate kuikata (Kiu) Na kama hakuna maji basi unaweza kumeza (Jora) zima la kitambaa upate japo ubaridi kwa wakati ule, Wakati ule hata ukikamata chuma basi kwa machungu yake unaweza kukipinda kwa jinsi ya machungu ya Roho inavotolewa, Macho yanakaribia kuruka kwa jinsi yalivotoka na dhiki unayoonjeshwa kuondoka kwako Ulimwenguni, Walokuzunguka machozi yanawatoka kwa taabu inayokufika, huku wanamaliza (Doti) za khanga kukufuta majasho yanomiminika kama mvua, na kama umeachwa peke yako wanakukuta chini ya uvungu wa kitanda unamkimbia (Malaika wa Mauti)
قُلۡ يَتَوَفَّٮٰكُم مَّلَكُ ٱلۡمَوۡتِ ٱلَّذِى وُكِّلَ بِكُمۡ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّكُمۡ تُرۡجَعُونَ
(Sema; Atakufisheni Malaika wa Mauti aliyewakilishwa kwenu, ikisha mtarejeshwa kwa Mollah wenu).
Yote haya yanakukuta kwa sababu ulipokua na Afya na nguvu zako ulikua hutaki mambo ya Mungu, hutaki kusikia hadith za Akhera, ukitajiwa mambo ya Dini unakunja uso au unacheka kuona upuuzi gani huu, pesa zako hazitoki ila kwenye mipira na pombe na anasa zengine, maskini hawana haki katika kipato chako, Mayatima hata nyuso zao huzitizami, maskini wanalala na njaa huku wewe ukinunua nguo mpya, dhahabu hazikutoshi, unapita kubadilisha na kuongeza magari, akikuuliza hali maskini unakereka, ulikua katika hali ya kuwafitini wenzio, kuwadhulumu na kuwasingizia mambo yasio ukweli, ulikua ukidhulumu nafsi za wenzio ili upate mafanikio ya kidunia, leo hii Hakimu wa Haki anaamrisha uyakabili mauti ukiwa katika hali ya mateso makubwa ili iwe ishara yako ya hayo makubwa zaidi unayokwenda kukutana nayo, ingia katika shimo lenye kiza kinene ukiwa huna muokozi, na hiyo ni yakini isiyo na Shaka. Tunamuomba Mollah wetu atunusuru na hali kama hiyo kwa kutusamehe na kutupa uongofu kabla ya kukutana na siku hii.
No comments:
Post a Comment