Sunday, December 30, 2012

SHEREHE ZA SIKU MPYA-PART-1

Asalaam Aleiykum,

Unakaribia wakati kwa baadhi yetu kupewa vidonge vya kulala na Muangalizi wetu wa malazi Shetani(Ibilis). Jee unawajua wale wanolala mwaka mpaka mwaka, Jee umejitizama kama na wewe umo katika hao walalao, Hao ni wale ambao wanaanda na kusheherekea mwaka mpya, wanajifunga kwa kuandaa makuku ya kuchoma, makatlesi ya samaki, chupa za whisky nk, na pia wale wanokwenda kununua vinywaji baridi kama juice na soda wote wanashiriki katika kuandaa malazi ya mwaka mzima ili wapate kumsahau Mollah wao kama anavo himiza (Ibilis)ili wapate kuamka (December 31)mwakani. Hawa wote wanatumia miezi yote 12 kutenda maovu na machafu kwa ajili ya kuhudhuria siku hii moja na kunywa hichi kidonge cha mwaka mpya.
Na cha kusikitisha zaidi wengi wetu katika Imani ndio tunashiriki sherehe hizi nini anatwambia Mollah wetu alipotutumia ujumbe kupitia kwa kipenzi chetu Bwana Mtume s.a.w. sura ya kahf aya ya 1-3,"ٱلۡحَمۡدُ لِلَّهِ ٱلَّذِىٓ أَنزَلَ عَلَىٰ عَبۡدِهِ ٱلۡكِتَـٰبَ وَلَمۡ يَجۡعَل لَّهُ ۥ عِوَجَاۜ "
"Sifa zote anastahiki Mwenye-enzi-mungu ambaye amemteremshia Mja wake kitabu,(Ambacho)hakukifanya kuwa na kwenda upande (upungufu).
" قَيِّمً۬ا لِّيُنذِرَ بَأۡسً۬ا شَدِيدً۬ا مِّن لَّدُنۡهُ وَيُبَشِّرَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ ٱلَّذِينَ يَعۡمَلُونَ ٱلصَّـٰلِحَـٰتِ أَنَّ لَهُمۡ أَجۡرًا حَسَنً۬ا "
"Kimetengenea vizuri(Kwa ukamilifu)ili kiwaonye watu adhabu kali itokayo kwake(Mollah wako)na kiwape habari njema wale wanoamini ambao wanafanya matendo mema, yakwamba watapata malipo mema"."مَّـٰكِثِينَ فِيهِ أَبَدً۬ا""wakae humo(katika hayo malipo)daima.
Wametajwa makundi mawili kwanza wale wanokwenda kujilaza wameambiwa nyie nendeni lakini kumbukeni kuna adhabu kali itokayo kwake ikiwa mtajilaza na kutenda maovu, na lile kundi la pili litakalo jizuia na kukaa macho likaelekeza imani zao kwa Mwenye-enzi-Mungu basi juu yao kuna malipo yasokatika yatadumu milele.
Haya mambo ya kuitikadi mwaka mpya ni wito wa Shetani(Ibilis)kama vile mnavoitwa kufunga Ramadhani na shetani ana siku yake nayo ni hii mwaka mpya, Na huizungusha shetani siku hii kwa sumu ya vivutio mbali mbali ili upate kwenda ukameze kidonge chake cha kulala mwaka mzima na kidonge chaweza kupenyezwa kokote ndani ya pombe au juice au kwenye chakula chochote, alaa usikatae mbona anakushawishi wala humuoni atashindwa kukutilia kidonge kwenye sambusa, sina haja ya kukutisha kasheherekee mwaka mpya halafu kama utaweza kuamka jitizame mwaka mzima matendo yako umekula kidonge au hujala.
Sasa nataka nifahamu vipi nalala mwaka mzima?
Inakuaje mwenyewe nakua sijui kama nimelala,
Kulala kuna tabaka(Level)3, Tabaka ya kwanza ni ile Unalala(Fofoo)umepotea kabisa hujui chochote umerejea kwa Mollah wako kwa ukamilifu, ndio maana ukiamka unajisikia fresh, umelala vizuri sana hujaota wala kusikia chochote, kulala huku tunaita kurejea kwa Mollah wako(1).Ama kulala kwa aina ya pili huendi kokote unabakia kwenye (Body)yako na hapo ndio tena unapata ndoto hizi na zile, huku ndiko kulala kwa aina ya pili(2). Ama kulala kwa aina ya tatu huku ni kulala ukiwa macho, na mifano ya kulala ukiwa macho ni kama vile maji yametoka(Kupwa) baharini akaja mtu kukuuzia kiwanja kwenye kando ya bahari maji yakirudi huna kiwanja, Au sasa hivi unasoma mawaidha haya lakini unakumbuka hadith fulani kwenye ile hadith ndio unakua umeamka na kwenye haya mawaidha utakua umelala, au mfano wengine ukenda kusali, kwenye ile sala unakua umelala na unaamka kwenye biashara jitizame wewe fikira zako zinakua wapi wakati unasali, na huku ndio kulala aina ya (3).
Na zaidi ya kulala huku kama vile unavo jilazimisha kwa unywaji wa pombe, usikilizaji wa Taarab ili upate kusahau kumbuka husahau tafrani zako tu bali unamsahau na Mollah wako, hizo ndio juhudi zako zote unazofanya ili upate kulala kwa mwaka mzima huku unakumbuka maasi na hicho ndio kidonge cha shetani na
 madawa ya kulevya yapo ya aina nyingi tizama ishara halafu utajijua umelala kwa kula kidonge cha mwaka mpya au uko macho, tizama wewe ukimkuta mkubwa wako anachukua rushwa jee wewe utaacha au utazidisha kuchukua, angalia ukimkuta Sheikh anatizama TV na huku kakwambia haramu wewe ukirudi nyumbani unaweza kuweka senema nzima,Shetani siku zote ana kuamsha kwenye maasi ndio maana na kutahadharisha kwenda kwenye sherehe hizo, Jitizame unavo kuwa mvivu kwenye mambo ya kheri sababu umelala, Angalia Ramadhani ikimalizika unavokua, unajua kwanini, sababu Ramadhan inakuamsha na mwanaadamu jambo la kuamshwa halipendi kabisa, ndio maana ikifika Ramadhani ya 29 wengine washalala kwa pombe na maasi mengine, sasa anokua macho anakua na hali gani, na Muumin anatakiwa asherehekee nini? kutaka kupata taaluma ya SHEREHE ZA SIKU MPYA, ENDELEA-PART-2

SHEREHE ZA SIKU MPYA-PART-2

Asalaam Aleiykum,

Anachotakiwa Muislam aliye Muumin wa kweli alojifunga na Mollah wake kwa dhati ya Imani basi sherehe yake itakua ya kila siku, na wala sio mwaka, katika maisha ya Muislam aliyekua macho kila siku ni sherehe kwake, akiamka kusali Alfajiri kwake ni siku mpya, jua linapochomoza kila kitu kinaamka na kuanza kutoa sauti, ndege wanaimba, mpaka jua lina raha zake likikuchoma, mpaka kuku wanazungumza lugha yao, kumbuka hakuna siku ilo fanana, kila siku ni tafauti na mwenzake.
Huoni tafauti jana ulikua unaumwa leo mzima, kitoto chako kimepiga hatua moja leo hii, mkeo jana kapika kile leo kapika hichi, leo asubuhi Asumini zimechanua, watoto wanakwenda school wamefurahi, mawingu jana yalikua meupe leo meusi, jana bahari ilikua imechafuka leo imetulia, jana nilisali msikiti fulani leo nasali na fulani, leo nimesikia sauti ya huyu jana nimesikia ya yule, paka wanagombana, jogoo anawika, hii ndio sherehe ya Muumin, hataki yeye mwaka mpya, kwake kila siku ni mpya na kila siku ni furaha, sababu yeye mwaka mzima yuko macho.
Na ukiwa utaziangalia hizo siku utagundua hazifanani kabisa, na kila siku ina mambo mapya, huna haja tena ya kusheherekea mwaka mpya kwani kwako wewe kila siku ni sherehe. Ila kama umelala ndio subiri December 31 ndio uamke kidogo ikisha ulale tena mpaka mwakani, lakini kama unataka sherehe ya Kiislam basi ipokee siku anayo kukirim Mollah wako, ipokee uienzi, angalia yote yanotokea kuanzia Alfajiri mpaka Magharib utaona pamejaa sherehe tupu, ndege wanashereheka,, vitoto vimefurahi, mpaka miti inashangiria. Na ukigundua hayo kuna siku pia itakuja utafunguliwa mengine na Mollah wako katika Rehma zake ili upate kuona mambo mepya katika ulimwengu huu unaoishi ambayo yapo lakini huyaoni kwa kuwa bado umelala, hebu tazama miujiza hii ili uione furaha ya maisha, hebu tazama ithbati hii umepewa nguzo tano na pia umeumbwa na vidole vitano haikujii chochote katika akili yako.
Hebu amka uifurahie siku na sio mwaka, hebu furahi sio kwa kujua vidole na nguzo tano tu bali na vyengine kama vitano hivi, hayo macho kupata kuona, masikio kupata kusikia, mikono yako kupata kugusa, pua yako kupata kunusa harufu, na ulimi kupata kujua ladha, hazitoshi kuwa sherehe za siku mpya juu yako, na ukisheherekea nguzo hizo tano basi utakua ni mwenye kushereheka na kila kitu katika maisha yako na wala husubiri mwaka mpya.
Nakutakieni kheri za siku mpya na furaha za kila siku.Namuomba Mollah atupe furaha za kila siku na tuzijue Rehma zake tunazo ziona na tusizo ziona Amin.

Monday, December 24, 2012

UISLAM NA MAPENZI YA MAISHA-PART-1

Asalaam Aleiykum.

Leo nataka niwaondoe wasiwasi na kuwajulisha wale wanopita kusema au kudhani kwamba Uislam unakwenda kinyume na Maisha na hutakiwi kufurahi kabisa, na huna unachokisikia ila vitisho tu, hakuna Maudhui ya upendo kabisa katika mengi ya maudhui yanayotolewa, Nadhani ukiwa na fikra hizo utakua hujapata kabisa maana ya Mawaidha au itakua usikivu wako unasikiliza maneno lakini sio mawaidha, ikiwa unasikiza maneno utakua kweli unapata vitisho kwani maneno yamjengwa kwa njia ya vitisho lakini maneno ni nyenzo inayotumika ili ukiyavuka maneno ukenda upande wa pili wa hayo maneno utakuta kusudio lenyewe nalo ndio dhumuni la kila Sheikh unayemsikiliza au Mwalim anayekusomesha anafanya kazi moja tu nayo kukurudisha katika hali ya kukumbuka "فَذَكِّرۡ إِنَّمَآ أَنتَ مُذَڪِّرٌ۬""Kumbusha hakika wewe ni mkumbushaji".
Hana haja Sheikh ya kutisha wala kukukamatia dini yako akawa anakuendesha anavo taka yeye, ukimuona Sheikh kama huyo anataka kukupangia kila jambo lako kutokana na muono wake basi mkimbie, elewa yeye mwenyewe haitambui dini yake na atakupeleka pabaya, kwani ndani ya dini hii husemwa hakuna kumlazimisha yoyote, " لَّسۡتَ عَلَيۡهِم بِمُصَيۡطِرٍ""Wewe si mwenye kuwatenza nguvu (Kuwalazimisha)".
Nimeona kuna haja la kulizungumza hili ili watu wasione Uislam unaenda kinyume na maisha haya, na Vipi Uislam utaenda kinyume na maisha, wakati ni dini ya haki na ukweli?. Kulijibu hili inabidi tujiulize tena nini dini?.
Dini ni mfumo mzima wa maisha ulojengeka kuanzia kuzaliwa kwako na kwenye afya yako pamoja na mambo yote yaliyomo kwenye Ulimwengu huu, au kwa Lugha ya ufupi(Dini ni Maisha)ya Muongozo wa kukuongoza katika furaha kwa njia ya haki na uadilifu ili yaweze kukupeleka katika hiyo hali kukumbuka(Ibadah)na kuelewa kuwa katika Ulimwengu huu yupo aloumba maisha haya na kuyapanga kama alivotaka mwenyewe na hakika yeye huyo anastahiki kushukuriwa kwa Rehma na Neema hii ya maisha alotupa waja wake, kwani mengine yote kinyume na atakavyo yeye jua yanakuongoza kwenye dhiki, mateso, na kuharibikiwa na hilo halina shaka kabisa.
Jeuri zote zinatupata pale tunapo sahau na kuwa hatujui jinsi gani bahati yako mwanaadamu baraka ilo kushukia ya wewe kuumbwa mwanaadamu, neema hii ya ufahamu hawakupewa viumbe vyengine vyote humu Ulimwenguni isipokua wewe, Wanyama hawajijui na wala hawana uwezo wa kurejea kwa Mollah, kwa matakwa yao wenyewe, lakini binaadamu kapewa uwezo akitaka anaweza kurejea kwa Mollah wake na fahamu zake bila ya kuharibika(Ndio maana wakati wa kufa unaambiwa useme-Laa-illah-illa-Allah)ufe huku unakumbuka na hiyo ndio Ibadah na huko ndiko kukumbuka, kwa hiyo kumbuka sana wakati unakata Roho uwe muangalifu wa kukumbuka (Kalimatul-Tawhid).
Sasa vipi Uislam unakubali mapenzi ya maisha, kwa mtu kustarehe katika ulimwengu huu, Endelea-PART-2

UISLAM NA MAPENZI YA MAISHA-PART-2

Asalaam Aleiykum,

Uislam ni dini yenye kukubali maisha ambapo anatakiwa Mtu aishi kwa ukamilifu, ndio maana utaona hukuti hata (utawa) katika dini hii unataka mapenzi ya Mungu fanya huku umeoa, una familia kila jambo limepangwa kwa kiasi na watu wameruhusiwa kufurahi, kuwa na mapenzi na ushirikiano ila yamewekwa masharti ukifurahi wewe uwe na uhakika walo wako,maskini,mafukara, wageni, wapita njia walopotelewa nao wanafurahi pia, pia unatakiwa katika hayo mapenzi yako ya maisha katika dunia hii ukumbuke pia kuna Upande wa pili ulio bora zaidi wa huu unaoitwa Akhera, anokumbusha ni yule yule alokupa maisha haya ya mwanzo na pia anachukua ahadi ya kukupa mara ya pili tena mazuri kupita haya.
Sasa wapi yametajwa haya Al-Imran aya ya 14.
"
زُيِّنَ لِلنَّاسِ حُبُّ ٱلشَّهَوَٲتِ مِنَ ٱلنِّسَآءِ وَٱلۡبَنِينَ وَٱلۡقَنَـٰطِيرِ ٱلۡمُقَنطَرَةِ مِنَ ٱلذَّهَبِ وَٱلۡفِضَّةِ وَٱلۡخَيۡلِ ٱلۡمُسَوَّمَةِ وَٱلۡأَنۡعَـٰمِ وَٱلۡحَرۡثِ‌ۗ ذَٲلِكَ مَتَـٰعُ ٱلۡحَيَوٰةِ ٱلدُّنۡيَا‌ۖ وَٱللَّهُ عِندَهُ ۥ حُسۡنُ ٱلۡمَـَٔابِ "
"Wanaadamu wamepewa huba ya kupenda wanawake na watoto na  (Wingi)wa Dhahabu na Fedha, na Farasi wanotunzwa vizuri, na wanyama na mashamba, na hayo ni matumizi ya maisha ya Duniani, na kwa Mwenye-enzi-Mungu ni kwenye marejeo mazuri"
Nafsi ya Mwanaadamu (Nature)yake imeumbiwa mapenzi, nikisema  neno mapenzi nina maana ya kupenda na kupenda ipo tafauti baina yake na mapenzi (Like na Love).
Nini kupenda?, Kupenda ni mkusanyiko wote wa  Raha na Furaha zote za ulimwengu huu, kupenda ni kama vile Afya tunajua ipo lakini hatujui kitu gani hiyo afya, na kupenda hali kadhalika tunajua tunapenda mambo mengi lakini hatujui kwanini tunapenda, na hayo yalotajwa katika hiyo aya ni machache ili kukupa yakini wewe Muislam kuwa una ruhusiwa kuwa na Mali, majumba, mashamba, nk, na hilo ndio umbile letu sisi wanaadamu imelazimishwa nafsi kuwa katika hali hiyo, ila unachotakiwa hapo usije kusahau ukawa mapenzi yako umekamatana na mali na majumba na madhahabu hata ukafikia kumsahau huyo alokupa haya maisha na hayo uloyapata.
Nini Mapenzi? Tafauti ya mapenzi na kupenda ni hii, kupenda umezaliwa nako(Nature)yako, lakini mapenzi ni kitu kinacholetwa baadae, ni zawadi ikiwa unastahiki kutoka kwa Mollah wako anakushushia(Kama ile aya ya Ndoa)inavosema ikisha tunajaalia Mapenzi na Rehma, na kwa njia ya rahisi ili upate kufahamu na kunielewa vizuri ni kama hivi, Kupenda ni kama Waridi, na mapenzi ni ile harufu yake, (Sasa fanya uchunguzi)mwenyewe ujue lipi linokuja mwanzo Waridi au harufu yake, pia napenda uelewe unaweza kulikamata waridi lakini huwezi kukamata harufu, harufu ndio kama mapenzi huna amri nayo inakuja yenyewe na inaondoka yenyewe, Unaweza kupenda kitu lakini usikipate, na unaweza kumpenda mtu lakini ukawa huna mapenzi naye, hiyo ndio maana yake.
Sasa tunarudi katika ile aya iliposema tumewafanya watu kuwa na huba ya kuwapenda wanawake, kusudio sio upande moja tu, ni pande zote mbili yaani kwa wanaume na wanawake ndio maana mwanzo ikatajwa watu, ilipowekwa khususia kwa kutaja wanawake ni kutokana na umbo la wanawake kuwa maridhiwa(Receptive)lakini katika jinsia wanawake wanawapenda wanaume na wanaume wanawapenda wanawake hakuna tafauti. Huo ndio mfumo wa Maisha ikisha ikaendelea aya na kupenda watoto, ili mfumo huu uwe wa mwenendo wa haki na maridhiano ndio ikawekwa mkisha kupendana mfunge ndoa, na mkifunga ndoa mtapewa zaidi ya hiyo kupendana, na hiyo zaidi ni hayo mapenzi na hizo Rehma ni hao watoto, na huo ndio mfumo wa haki na uadilifu unaotakiwa wa kuwapenda wanawake na watoto, na hizo Rehma zitaendelea kwa kupewa zaidi na zaidi hayo marundo ya dhahabu na fedha, na mafarasi, si lazima upewe mafarasi usije kusema mbona siyaoni hayo mafarasi, pengine wewe umepangiwa umiliki kuku, na hiyo ndio kadara uliyokusudiwa, sasa ukianza kushindana kuyatafuta mafarasi matatizo ya maisha yanaanzia hapo unakua huna furaha hupendi kitu, kila wakati umekunja uso, sababu unashindana na yule alokupangia, ukiwa na kidani kimoja shukuru usishindane ukataka upate bangili ishirini, na ukishukuru utaona huna habari kabisa na hayo madhahabu mengi, na pia msishangae na wale wanopenda wanyama, ikawa unamcheka anompenda paka, au mbwa, kuanzia leo jua yule ndio maumbile yake na wewe pia unavyo unavo vipenda unavijua mwenyewe, mwengine anapenda shamba lake anaona raha kulima na kupanda mazao yake, mwengine anapenda gari yake, mwengine anapenda nyumba yake na mapambo yake hakuna kosa katika hilo, ila msisitizo usije kusahau alo kupa uwezo wa maisha hayo, na haikatazwi kwako kuomba mazuri uyapendayo kutoka kwa Mollah wako, lakini utakua na Imani kubwa na unyenyekevu iwapo utaridhia na kusema "Ewe Mollah wangu weye ndie Uloniumba na wewe ni mwenye kujua mahitajio yangu, basi naomba nipe kama ulivo nipangia wewe  katika hizo raha na mapenzi ya maisha haya, nifanye mimi kuwa maridhawa kwa chochote kile kijacho katika maisha yangu, ukinipa raha na starehe nipe na afya nipate kufurahi na huku nakukumbuka weye, na utakaponipa shida na matatizo, basi nipe na ustahamilivu na shukurani huku nikikukumbuka weye Mollah wangu. Amin.

Saturday, December 15, 2012

DIRISHA LA ROHO- PART-1

Asalaam Aleiykum,

Imekufikia habari pale jambazi au mwizi anapo chungulia dirishani ndani ya nyumba yako? Hali gani inakutokezea, Jee unajijua unavo hangaika kuweka madirisha ya chuma na walinzi, Na usingizi sasa hupati tena. Basi elewa pia hali kama hiyo inakutokezea iwapo mtu atakutizama machoni, Hujioni wewe unavotaka kupigana, unamfata mtu na kumuuliza wewe unanitazamia nini namna hiyo, Umepata kujiuliza kwanini unakua mkali hali hiyo?.
Leo nakupeleka katika siri ilofichika ndani ya macho yako na kama ukiwa mwerevu ukaigundua siri hii basi mafanikio yako yataanzia hii leo, mada hii itakubadilisha kabisa mtazamo wako ulokua nao siku zote. Kwanini nikalizungumza hili la dirisha la Roho, sababu kubwa naona huruma nikitizama macho ya watu na kuona dalili za mateso kila mmoja wetu ana mizigo alobeba kifuani mwake na akawa hajui au hana njia ya kuitua mizigo hiyo.
Wale walosema yakua Mwili wa Mwanaadamu ni nyumba ya Roho basi pia haitokua shaka na haya Macho tulokua nayo kuwa madirisha yake. Sasa kwanini nikayaita madirisha?Nimeyaita madirisha kwa kuwa nyuma ya hayo Macho yako kuna Mtu anachungulia na uthibitisho utaupata kwenye hii sura ya Qiyama aya ya 14."بَلِ ٱلۡإِنسَـٰنُ عَلَىٰ نَفۡسِهِۦ بَصِيرَةٌ۬"
"Bali Mwanaadamu ni Shahidi wa nafsi yake"
Sasa kutaka upate yakini nenda kwenye kioo ukajitizame utaona unajiona sura yako, na hayo macho yako unayaona, sasa jiulize nani huyu mwenye kuona hivi vyote?. Katika safari hii ya kuchungulia ndani ya Madirisha hayo kusudio langu ni kukufahamisha mwenzangu vipi utaweza kusafisha macho yako na kupunguza mizigo iliyomo ndani ya kifua chako ili usije ukawa unabakisha makorokoro mengi yaso faida ndani ya hilo Jumba(Nafsi)yako.
Usije kushangaa mbona sijapata kuyasikia haya, ni vizuri hujapata kuyasikia sasa tulia upate kuzinduliwa katika somo hili la  (Tawhid)na nafsi yako ili upate kupiga mbizi ndani ya bahari hii ya (Sprituality) ENDELEA PART 2

DIRISHA LA ROHO-PART-2

Asalaam Aleiykum,

"وَلَوۡ أَلۡقَىٰ مَعَاذِيرَهُ ۥ "
Japo anatoa udhuru(Sababu)
Wacha kujivika shungi ukawa unajificha siku zote hutaki kuyajua haya, Acha kutafuta mawaidha ya kukulaza ukawa kama mbuni unajifunika uso wako kwenye ardhi, nyanyua uso kabiliana na ukweli huu nani huyu anotembea akajiona?, nani huyu mwenye kuiona mikono na miguu na viungo vyengine?, nani huyu hata nikiwa nimelala naona ndoto zangu?, huyu mwenye kuona khassa nani? Ewe ndugu yangu jiulize maswali haya kabla ya kuulizwa, jijue kabla ya kujulishwa, ondosha sasa porojo, ondosha sasa maskhara wakati unapotea na wewe unaendelea kuleta nyudhuru unazidi kuzama katika mambo ya kujisahaulisha.
Wanataaluma ya sayansi wanatwambia kuwa Mwili wa mwanaadamu una lugha yake makhsusi(Body language)ambayo unaweza kumjua mtu kakusudia nini na ukisema uongo wanajua, basi na vile vile wanataaluma ya dini wao wamegundua mwanzo kuwa kutokana na macho yako pia wanaweza kujua nini kimekusibu. Hata wewe mtu wa kawaida unaweza kuyajua hayo hebu katizame macho ya mgonjwa na yako uijue tafauti, Ikisha ukimaliza katizame macho yako na ya mtoto mdogo au ya yule mtu alotulia kwa ghushui ya mambo ya kidini mja wa Mwenye-enzi-Mungu, Hapo utaona macho ya watoto na wacha Mungu hayana tafauti yanangara yanatoa(Sparkling)nuru yanameremeta na huku yamejawa na machozi ya unyenyekevu. Lakini maskini macho yetu kwanza makavu, ikisha yamekosa nuru ishatoweka kwa sababu ya mizigo tulobeba, macho mekundu kila unayemuona wasema ni adui yako, yeye anakuogopa na wewe unamuogopa, mkitizamana mara moja tu hamuangaliani tena kila mmoja anamtisha mwenziwe.
Kwanini inakua hivyo? Sababu kubwa Roho nayo inahitaji kula na Macho na Masikio ndio midomo (Milango)yake, Sasa mtizame Muislam anailisha nini Roho yake hata akafikia hali hiyo, Hukuti anachoingiza ndani ila kajaza majina ya (Khanga)zote anayajua yeye, Habari zote za mitaani kahifadhi yeye, mambo yote ya Ulimwengu yamejaa kifuani mwake na mbali na matatizo yake mwenyewe, ndio maana unamuona mtu kachoka ukimtizama machoni na wala hataki umtizame mara ya pili, hii ndio hali sote tulokua nayo na ni baadhi tu ya mizigo iliyomo ndani ya nafsi zetu.
Macho yanaonesha huzuni, macho yanaonesha sasa unabeba mizigo ya ziada na ukitaka kuijua ENDELEA PART 3

DIRISHA LA ROHO-PART-3

Asalaam Aleiykum,

"إِنَّا خَلَقۡنَا ٱلۡإِنسَـٰنَ مِن نُّطۡفَةٍ أَمۡشَاجٍ۬ نَّبۡتَلِيهِ فَجَعَلۡنَـٰهُ سَمِيعَۢا بَصِيرًا"
"Hakika tumemuumba mwanaadamu kutokana na mbegu ya uhai iliyo changanyika, ili tumfanyie mtihani(Mtihani kwa amri zetu na makatazo yetu)tukamjaalia mwenye kusikia (na)kuona."
Sasa jitizame wewe wala usisubiri mpaka ukaletewa kitabu chako, unaweza kukiona sasa hivi, leo moja jiangalie mizigo ipi kwa siku unayopeleka ndani ya Roho yako, jiulize katika mizigo hii inangia japo aya (10)za Quraan humu ndani, jawabu laa, jee yanaingia mambo ya kheri humu ndani, laa, ukijitizama kwa uyakinifu utajikuta mpaka unakwenda kulala kilichoingia ndani ya Roho yako ni michezo ya senema au mipira, nyimbo za taraab au disco, Mambo ya watu au habari za uongo, maudhui ya siasa au mambo ya kipuuzi na kama utarejeshewa kaseti yako ya leo basi unaweza kwenda mbio, kumbe ndio hivyo ninavyoishi, haya ndio machafuzi ninayo peleka ndani ya Roho yangu, hee mbona zimejaa picha za bendera za chama basi hamna hata picha moja ya makka, ina maana humu ndani mimi sitii chochote cha kheri.
Nilikua simshukuru Mollah wangu alonikirimu huu Uhai nikaweza kuangalia yaliyo ya kheri, sikumbuki mimi kwamba wakati wowote anaweza kuchukua Uhai wake nikawa si chochote bali ni dongo linalofukiwa katika ardhi na huku mimi nalishuhudia. Ewe Ndugu yangu zinduka ujue thamani ya uhai wako, unajua kama thamani ya uhai wako ni sawa sawa na gilasi ya maji inayotolewa bure, jee unayo habari hii!! Unajua kama ukiwa jangwani umebanwa na kiu akaja mtu akakwambia baina ya Uhai wako na mali yako yote na mkeo na wanao na kila ulichonacho thamani yake ni sawa sawa na haya maji unataka niachie mimi hivyo vyote na wewe chukua hii gilasi ya maji unajua kama utatoa bila ya kujishauri.Sasa ikiwa Gilasi ya Maji ina thamani kuliko mali yako, kuliko Uraisi wako, Kuliko Ubunge wako, Kuliko Ubalozi wako, kuliko Utajiri wako kuliko Cheo chako, kuliko vyote ulivyo navyo basi kwanini humfati huyu mwenye maji, kwanini huanzi safari ya kwenda kwa mtoa maji buree bila hata ya ndururu, kwanini hufati amri zake na makatazo yake. Ikiwa maji thamani yake hii nini habari yetu sisi ya hayo mengine ya jicho halijawahi kuona na sikio halijapata kusikia.
Umepewa hayo Macho na masikio ili upate kuongoka na kushukuru basi yatumie kwa kutizama mambo ya kheri, kusikiliza mambo ya kheri, utende mambo ya kheri hilo ndio dhumuni la kuumbwa kwako, lakini wee, kilichomo ndani ya roho yako ni kero tupu, ndani umejaa matamanio, ukimtizama mtu unaanza kupanga nikimpata itakuaje, itakua jinsi kadha wa kadhaa, halafu itakua vile na hivi, na kama ghafla litaondoshwa pazia tuone una fikiri nini tutaona senema nzima ya mchezo wa maasi, haya ndio tuloyajaza ndani ya Roho zetu, kama si utajiri kiburi, kama si uongo rushwa, macho yanaonesha maradhi sisi na wagonjwa hatuna tafauti, tafauti ni ndogo sana wale wanaumwa mwili, na sisi wengine tuna maradhi ya roho, sasa Mwanaadamu ufanye nini?ENDELEA PART 4

DIRISHA LA ROHO-PART-4

Asalaam Aleiykum,

Quraan Noor aya ya 30

"قُل لِّلۡمُؤۡمِنِينَ يَغُضُّواْ مِنۡ أَبۡصَـٰرِهِمۡ وَيَحۡفَظُواْ فُرُوجَهُمۡ‌ۚ ذَٲلِكَ أَزۡكَىٰ لَهُمۡ‌ۗ إِنَّ ٱللَّهَ خَبِيرُۢ بِمَا يَصۡنَعُونَ "
"Waambie waislam wanaume wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, hili ni takaso kwao, Mwenye-enzi-Mungu anazo habari(zote)za wanayoyafanya".Na pia aya inayofatia ya 31 wanatajwa wanawake kwa maelezo hayo hayo ya hapo juu isipokua yameongezeka ya ziada kwa ajili ya ruhusa za wanawake:
Yalo katazwa yapo mengi sina haja ya kuyataja yote kwa kuwa mimi niko katika maudhui ya kukumbusha nipe nafasi niendelee japo kidogo nikupe hii maana ya kuangusha macho ili ujue kuna kuwaje huko kutakaswa(Kusafishwa, kushushwa hiyo mizigo)unayojitwisha Rohoni mwako.
Katika kutizama kuna mambo mawili yanafanyika la kwanza(1)Unatoa ita upendavyo(Energy au Light)kwenda nje, nadhani utakua ushapata ujuzi wa hiyo (Light)kwani ukifikicha macho si unaona nyota nyota zinaelea kwenye macho yako. Na la pili(2)ni (Reverse process)unarudisha(Information)ndani kile unacho angalia kinatoa (Energy-Light) yake kuja kwako, sasa kama ikiwa hicho unacho angalia ni mambo ya matamanio basi zinatumika nguvu zaidi za kutizama(Kupeleka kwa kuona)na kwa (Kurudisha)ndani ndio maana ukaambiwa angusha macho, jihifadhi na hifadhi tupu yako kwani hicho ndio kina kumaliza kabisa, huo ni mfano mmoja tu nilo utaja kwa ufupi na mifano ipo mingi tu.
Hiyo mizigo ya nguvu nilizo zitaja ndio inokwenda kujaa humo ndani ya kifua chako, na zikishamiri sana hazina pahala pa kukaa inabidi sasa nguvu hizi  zitoke nje, na zikitoka nje ndipo hutoa ishara zake, na ishara zake ni hizi.
Jitizame wewe kama unapenda mali hali yako inakuaje ukiona mali za watu, kama unapenda pesa vipi unakua ukitajiwa mambo ya pesa, kama una mahamaki vipi unakua ikiwa utachokozwa kidogo, kama unapenda wanawake au wanaume jitizame vipi unavo hangaika ukiona watu wamechonga nyusi na kope zao, kama unapenda habari za watu jiangalie unavozitafuta habari hizo, ikiwa mpenzi wa uongo jitizame ustaadi wako wa kupanga na kugeuza mambo, kila kilojaa katika Roho yako basi na jinsia yako inageuka kuwa mjumbe wa hilo tendo, na hali hiyo inaendelea kujaza daftari lako la Akhera.
Sasa ufanye nini? Umepewa (Simple technic)mbinu au nyenzo ya kuyaepuka mizigo hiyo, umeambiwa angusha macho yako, ukiona mambo yasofaa(Simple)geuza uso kama huwezi kuangusha macho, ikiwa umepandwa na hamaki jitizame ndani kwanini nimehamaki, wewe una uwezo wa kuona nje kwanini usiwe na uwezo kuona ndani, Ukiona mali sema moyoni kwanini unaipenda mali isokua yangu,ukiona matamanio jisemeze kwanini natizama, ukiweza kufanya hivyo ukajigundua tabia yako isofaa kwa muda wa mwezi mmoja utakua unaanza kushusha hiyo mizigo taratibu tena yote hata ulobeba zamani, na utaanza kusikia raha ya maisha inakuteremkia na utaona wepesi mkubwa katika Roho yako na hapo ndio zinaanza hizo ishara za Utakaso ulotajwa, mapenzi yataanza kukushukia ndani ya Roho kwa njia ya ajabu.
Ewe Ndugu Muislam punguza mizigo uishi maisha ya raha,huna haja ya kuteseka kama unavoteseka hivi sasa, yakiondoka madhila hayo Mwenye-enzi-Mungu anakujaza Rehma zake inakua kama ulopewa ile gilasi ya maji jangwani tena yalo bariidi. Namuomba Mollah Karima atujaalie kuweza kushusha mizigo yetu bila ya kuchelewa, Namuomba Mollah atufungulie fahamu ili tupate kuyafahamu haya tunayo fahamishwa.Amin.

Saturday, December 8, 2012

MAISHA YA KIDINI-PART 1

Asalaam Aleiykum,

Leo tunaingia katika Maudhui hii ya Maisha ya kidini tukiwa na tamaa kila mmoja wetu kupata angalau japo kwa uchache kuishi kama maamrisho ya kidini yanavo himiza, Kwanini tunatamani?.
Tunatamani kwa sababu (Nature)yetu ina tutaka tuishi hivyo, Dhumuni la kuumbwa kwetu linasisitiza tuishi kwa mwenendo huo, lakini imekua hasara kubwa, imefikia hasara yenyewe katika kila watu mia (100)basi unapata watu wawili tu ndio wenye kuishi maisha ya kidini, na sababu kubwa yule mwenye kuishi maisha ya kidini hawezi kuhadithia kwani akihadithia hakuna ato muamini na wengine wanaweza kusema sasa mambo tayari, apelekwe mirembe au kidongo chekundu huyu kesha, akili zisha haribika, ndio maana wenye kuishi maisha haya wamenyamaza kimya wanaendelea kutumia utajiri wao waloupata na ufalme wao uso kuwa na kikomo.
Hawa wanoishi maisha haya kwao hakuna kuteseka, hamna machungu, hamna kujuta kila siku wanapoamka ni furaha tupu, kwa ajili ya  Neema itokayo kwa Mollah wao, hawana kero za Akili wala lawama za wanaadamu.
Sasa inakuaje wachache sana kuyapata maisha haya? na kama raha hizo zote na furaha zinapatikana kwanini wengine hatuwezi kuyapata maisha haya?. Naam Maisha haya ni magumu sana kupatikana na pia rahisi mno iwapo utaamua kuyataka. Nini tafauti yake?
Tafauti yake ni ndogo tu, kwamba bado hujaingia dini Kikamilifu, usije ukajisumbua na kusema mbona nasikiliza mawaidha sana, mbona nasoma Quraan vizuri, usije ukasema navaa hijab siku zote na hayo yakakufanya uamini sasa unaishi maisha ya kidini, lisije likakusumbua sijida kuubwa ukaona sasa nimeshazama kwenye maisha ya kidini, bado kabisa, ndivo vizuri unajitahidi lakini bado unatakiwa uzidishe juhudi na ubadilishe mwenendo wako na hii ndio madhumuni ya mada yetu ya leo, ili kukupa mawili matatu yapate kukuchukua kukupeleka kwenye hayo maisha ya kidini.
Sasa ufanye nini?kuyapata maisha hayo msikilize Bwana Mtume s.a.w kasema nini kuhusiana na kuishi kidini,"Alionesha kifuani mara tatu na kusema Ucha Mungu(Taqwa)uko humu ndani"Alikua na maana gani? Maana ilokusudiwa hapo hakuna nyengine ila kutakiwa Mja urejee ndani, unatakiwa uingie katika nafsi yako(peke yako)ujiulize jee naishi maisha ya Kidini?. Jee nimeingia dini yangu kikamilifu? .Sura ya Baqarah aya ya 208,
"يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ ٱدۡخُلُواْ فِى ٱلسِّلۡمِ ڪَآفَّةً۬ وَلَا تَتَّبِعُواْ خُطُوَٲتِ ٱلشَّيۡطَـٰنِ‌ۚ إِنَّهُ ۥ لَڪُمۡ عَدُوٌّ۬ مُّبِينٌ۬
  "Enyi Mloamini ingieni katika hukumu za Kiislam zote,(Kwa ukamilifu)Na wala msifate nyayo za Shetani, Hakika yeye kwenu ni adui alo dhahiri".
Vipi utajijua umeingia kwenye hizo hukumu, hapo ndipo pagumu kwanza lazima uondoshe nyayo za Shetani kwani japo una sali na kuomba dua lakini baada ya kwenda kulia wewe unafata nyayo za shetani kuelekea kushoto, Sasa vipi utazikimbia nyayo za Shetani.
Endelea part 2

MAISHA YA KIDINI PART-2

Asalaam Aleiykum,

Vipi nitaziepuka nyayo za shetani ili nianze kuishi maisha ya kidini, nifanye nini hata namie nipate hazina hii ya kidini, vipi nibadilike kuelekea katika Maisha alo yaridhia Mollah wangu, sasa bora nijitizame nimeshaanza kubadilika kueleka kwenye huo ukamilifu wa hukumu, huwezi kufanya yote hayo mpaka kwanza hamaki ziondoke, huwezi kuishi maisha ya kidini ikiwa katika moyo wako kuna japo chembe ya chuki, jiulize jee mimi naweza kusamehe nikikosewa?Mbona nina wivu? kwanini nina hasira?mbona moyo wangu una husuda?mbona sipendi watu bure pasi na kosa lolote?kwanini maneno madogo tu yananifanya nigombane na mwenzangu maisha, Mbona mkali kwa mke wangu au mume wangu?, kwanini mpaka watoto wangu wananiogopa? Kumbuka matatizo yote haya yamo ndani ya nafsi yako, vitu hivi vyote vimo kifuani hapo aliposema Bwana Mtume s.a.w sasa (Taqwa)itakaa wapi?, vipi utaweza kuyapata maisha ya kidini, kuyapata maisha haya lazima kwanza ujisafishe, Kwani hapo kifuani mfano wake kama maji yaliyomo mtungini, na mtungi tunaujua ukiutingisha au kuutia kata basi maji yanatibuka na hali kama hiyo ndio inayotokea kwako wewe.
Maisha ya kidini ni magumu kwa sababu sote tunaishi nje ya kifua, kinyume na maagizo ya Bwana Mtume s.a.w, tuishi ndani ya kifua,  ndio maana tunakabiliwa na ugumu wa kuishi kidini kwa sababu sote tumo kwenye mashindano ya kila siku, lazima ujenge jumba la kifahari, lazima uwe na gari nzuri ya kumshinda fulani, huwezi kuwa na furaha mpaka utajirike, sasa kama una matamanio hayo yote ya nje unataka hichi na kile lazima uvipate vipi utayapata maisha ya kidini. Kifua chako kimejaa matakwa ya kidunia na huku unataka maisha ya kidini, hapo dini haiwezi kuingia ndio maana utaona Sala zote ni za kuonesha watu, kila kitu chako lazima watu wakishuhudie, ukisali peke yako unasoma sura fupi kisha huyo unakimbia lakini ngoja akugonge bega mtu huko nyuma yako unaweza kusoma nusu msahafu hujijui unamsalia Mungu au binaadamu.
Bwana Mtume s.a.w alipoashiria kifuani mwake mara tatu alitaka Umma wake urejee ndani, Ili kila mmoja apate kuishi maisha ya kidini, Maisha yenye kufuzu. Mpaka sasa hivi unasoma maisha yako na yangu sote tunaishi nje, awe Sheikh, au Mwanafunzi, Imam au Maamuma sote sawa bado hatujui vipi kuishi maisha ya kidini yaliyomo vifuani mwetu, na ukichunguza hakuna hata Mmoja mwenye furaha sote tumejishughulisha na kuchuma mali, tunafukuzia kutafuta pesa, Labda mtu maradhi yake umaarufu, wengine wanataka cheo ndio waridhike, mwengine ataka aonekane yeye mzuri, na Mbaya zaidi ni yule anotaka aonekane yeye Mcha Mungu, na wengine wanaweka shuruti lazima nipate kitu fulani ndio nitakua furahani, ukiwa na hali hizo na zengine mfano wa hizo basi jijue unaishi nje ya kifua chako. Ama yule alokua hana shuruti lolote lile na tayari kasharejea kwenye kifua chake huyu anakua kashaisoma aya hii.Endelea part 3

MAISHA YA KIDINI PART 3

Asalaam Aleiykum,

"وَفِىٓ أَنفُسِكُمۡ‌ۚ أَفَلَا تُبۡصِرُونَ"
"Na katika nafsi zenu jee hamuoni"
Mwenye-enzi-Mungu ana tutaka tujiangalie ndani ya nafsi zetu, tukisha jiangalia na kujisafisha utakutana na utajiri mkubwa usokua na mfano wake, "Ewe mwanaadamu jitizame nafsi yako utagundua utajiri mkubwa sana na kama huelewi basi haitoshi hii afya kuwa dalili kwako.
Vipi ujitizame, jitizame sababu bado unaishi nje, sasa wacha nikupe mifano ili uitizame humo ndani upate kujibadilisha, kumbuka zoezi hili la mwanzo vitu unoweza kuvitizama ni hivi, Wivu, Chuki, Hasira,Hamaki,Huruma,furaha, na Mapenzi vyote hivi vimo ndani ya nafsi yako, Basi hebu chukulia mfano huu, Mwanao kafanya kitu kimekukera, jambo la mwanzo wewe hutizami ndani ya nafsi yako ila unatizama nje kwenye hiyo kero yenyewe, na hiyo kero pengine ni maneno tu yule mtoto kakujibu au Mkeo basi kama utaachiwa unaweza kupata (Heart-Attack)kwanini kwa sababu unaishi nje, hebu rejea ndani umekerwa sasa jiulize nini kinatokea ndani ya nafsi yangu, kwanini nakereka hizi hamaki ni kitu gani, jee hichi kitu cha kunihamakisha, basi ukiweza kufanya mara mbili tatu ukawa unakumbuka kuitizama nafsi yako utaanza kuona kitu kipya kinatokea juu yako itakua hamaki zikitokea na mtazamo unatokea na ukiendelea na zoezi hili itafika wakati kabla ya hamaki kutokezea mtazamo ushafika, Na hapo tena unakua ushaanza kubadilika unakua na uwezo wa hamaki kuzigeuza huruma na ukiweza kufanya hivyo ushaanza kuishi maisha ya kidini utaanza kupata upole ambayo inafatia na Imani, hapo tena maisha yanabadilika moja kwa moja.
Na kama una wivu basi pale tendo la wivu linapotokezea wewe usitizame nje kwenye tendo jitizame mwenyewe ndani huu wivu ni kitu gani nini kinatokezea, ukiweza kufanya hivo basi kinachotokezea hapo ni mabadiliko ya wivu kugeuka mapenzi,Vipi?Utajiuliza vipi wivu ugeuke mapenzi wakati mie nampenda ndio nikaona wivu, Jawabu Naam wivu si mapenzi, wivu ni sumu ya kutaka kukikamata kitu kisikutoke mpaka kile kilokamatwa kinaanza kusikia dhiki. Basi irejee tena kuitizama hamaki, hamaki haikai nje ila inakaa ndani ya kifua chako, kama maji yalivo mtungini ukiyatia kata yanatibuka, ndio maana na wewe mtu anafanya jambo nje lakini unatibuka ndani, Bwana Mtume s.a.w kasema"Ukipandwa na hamaki basi kaa kitako", Maana yake? yatulize maji, wewe chunguza ukikaa kitako hamaki zinapungua au kutoweka kabisa, au jaribu ukishikwa na hamaki badilisha mazungumzo utaona hamaki inatulia hata hujui inakwenda wapi(Basi katika nafsi zenu hamuangalii)basi kuanzia leo ukipandishwa hamaki jitizame ndani ya nafsi yako nini kinatokea, utagundua kuna(energy)fulani inatembea na ukiendeleza zoezi hili kwa muda wa siku 90 utakuja kuona kabla ya hamaki kufika unatangulia wewe muangaliaji, na muangaliaji akiweza kumudu kuvishudia vitu viwili vitatu katika nafsi yake tayari anaishi maisha ya kidini, hapo ukitaka kujionesha huwezi tena utakua unajisuta mwenyewe ndani kwa ndani, utakua hutaki tena yale maisha ya nje niloyataja mwanzoni na hapo ndio unafunguliwa Ilham ya kuishi kama inavotaja aya hii.Endelea 4

MAISHA YA KIDINI PART 4

Asalaam Aleiykum,

"إِنَّ فِى خَلۡقِ ٱلسَّمَـٰوَٲتِ وَٱلۡأَرۡضِ وَٱخۡتِلَـٰفِ ٱلَّيۡلِ وَٱلنَّہَارِ لَأَيَـٰتٍ۬ لِّأُوْلِى ٱلۡأَلۡبَ()ٱلَّذِينَ يَذۡكُرُونَ ٱللَّهَ قِيَـٰمً۬ا وَقُعُودً۬ا وَعَلَىٰ جُنُوبِهِمۡ وَيَتَفَڪَّرُونَ فِى خَلۡقِ ٱلسَّمَـٰوَٲتِ وَٱلۡأَرۡضِ رَبَّنَا مَا خَلَقۡتَ هَـٰذَا بَـٰطِلاً۬ سُبۡحَـٰنَكَ فَقِنَا عَذَابَ ٱلنَّارِ "
"Hakika katika kuumbwa mbingu na ardhi na (katika)kutafautisha usiku na mchana, ziko alama kwa wenye Akili".Ambao humkumbuka Mollah wao wakiwa wima na wakikaa na wakilala, Hufikiri umbo la mbingu na ardhi, (husema)Mollah wetu huku viumba hivi bure, Utukufu ni wako, Basi tuepushe na adhabu ya Moto".
Hapa lazima ieleweke kukumbuka sio kule kusema Laa-Illah-Ilah-Allah kwa maneno, bali kusudio lake ni kuishi na Mollah wako nyakati zote ukiwa kazini unafanya kazi zako, Basi uwe unajua Mollah wako yupo moyoni kwako unamkumbuka kama hivi, Mollah wangu kanipa afya leo naweza kutekeleza kazi yangu, Mollah wangu kanipa ujuzi nafahamu kazi yangu, Mollah wangu kanipa maarifa naweza kufanya Biashara, Mollah wangu yu karibu na mimi ananinusuru na mambo mengi, ana ni Ruzuku fahamu hii ya kuweza kumkumbuka na kutekeleza wajibu wangu, yeye ndie alofanya nipandishwe cheo hichi, sasa ikiwa kazi ya kukaa au kusimama au umepanda farasi au gari basi mote humo unawajibika kumkumbuka Mollah wako, ikiwa umeweza kukumbuka hamaki, hasira na mengineyo huwezi kumsahau Mollah wako, na ukiipata Rehma hiyo wewe sasa unaishi Maisha ya Kidini, lakini huwezi kufikia hapo mpaka upitie kujisafisha na kujizoesha kuwa Muangaliaji wa hiyo nafsi kama nilivo taja huko nyuma. Sasa Ukishaanza kuweza kumkumbuka Mollah wako hapo tena ndio utakua na uwezo wa kuanza kufikiri kuumbwa Mbingu na Ardhi na kujua yote haya hayakuumbwa hivi hivi kuna sababu zake unaanza kugundua tena siri za Ulimwengu usije kujishughulisha sasa hivi wakati Mti ulo jirani yako huufikiri utafikiri nyota ilo Mbinguni?basi tena inakutoka ile dua ya Rabbi niepushe na adhabu ya Moto na safari hiyo ya ugunduzi inakuchukua unakua daima umo kwenye furaha, unakua ushagundua hazina iliyomo kwenye nafsi, na huo ni utajiri mkubwa ambao hausemeki na shuruti lake urejee kwenye kifua ukakutane na hiyo (Taqwa)hapo ndipo kwenye utajiri wa kuwashinda matajiri wote.
Na mwanzoni niliposema ni vilevile Rahisi kupata Maisha ya kidini nilikua nakusudia watu wa aina hii Quraan Baqarah 207.

"وَمِنَ ٱلنَّاسِ مَن يَشۡرِى نَفۡسَهُ ٱبۡتِغَآءَ مَرۡضَاتِ ٱللَّهِ‌ۗ وَٱللَّهُ رَءُوفُۢ بِٱلۡعِبَادِ" 
Kuna katika watu, wauzao nafsi zao kwa kutaka radhi za Mwenye-enzi-Mungu, Na Mwenye-enzi-Mungu ni mpole kwa waja wake.
Unaweza kuyapata maisha haya ya kidini kwa urahisi ikiwa utaondosha Kiburi, Utaondosha Ubinafsi, na usidhani vitu hivyo ni rahisi kuviwacha mara moja, sababu toka utotoni vimeshaota mizizi katika nafsi yako siku zote unatizama nje mara ghafla unaambiwa utazame ndani, ndio maana nikasema vigumu kuyapata maisha ya kidini japo tunayatamani, tizama mifano Sheikh anatoa mawaidha akisha kumaliza ukimfata pembeni kumuomba pesa ya kula tu hakupi japo yeye kazungumzia kuwalisha maskini, sasa kwanini inakua hivyo, sababu yeye mwenyewe hajabadilika anazungumza maneno tu lakini ndani hajajitizama kabisa wala hajui kumekaaje, na kama unabisha mkere kidogo akimaliza kuhutubia utaona hamaki zake zinamshinda jambazi, sababu ni ile ile bado hajabadilika, ninacho sisitiza mimi kwanza jisafishe, ondoa wivu, ondoa chuki, ondoa hamaki, ondoa uadui, ondoa choyo. ondoa hasira, vikiondoka vyote hivyo kifuani kwako utajikuta ghafla umefunguliwa mlango wa hekima, mwenendo wako utabadilika, matendo yako yatabadilika, yatakua sio ya kujilazimisha bali yanatokezea yenyewe kwa desturi ya kidini, utaanza kuona dalili ndogo ndogo  zinajitokeza, mtu akikuomba kitu ukimnyima basi utasikia uchungu siku ya pili hata mlevi akikuomba utampa, na huku unasema Mollah wangu umemleta huyu kuja kunijaribu mimi, sikua mimi mwenye kuweza kumnyima.
Utakua unaona ikisomwa Quraan unasikizia kifuani si masikioni tena na huku machozi yanakutoka, ukiona dalili hizo basi jijue sasa tayari ushaingia katika maisha ya kidini, hapo uanze kuwa makini usiruhusu tena mambo ya kipuuzi kuyashiriki(وَٱلَّذِينَ هُمۡ عَنِ ٱللَّغۡوِ مُعۡرِضُونَ)utaanza kuacha kutizama mambo ya kipuuzi puuzi na yasio maana, utakua husikilizi mambo ya kipumbavu pumbavu na ukiweza kuishi katika maisha ya dini basi mpaka kufa kwako mwili utazeeka lakini wewe ndani utabaki(Fresh-Inside)(إِلَّا ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَمِلُواْ ٱلصَّـٰلِحَـٰتِ فَلَهُمۡ أَجۡرٌ غَيۡرُ مَمۡنُونٍ۬ ) na hiyo ndio njia ilonyooka Mollah wetu atujaalie kwa sote tuipate, Isiwe mawaidha kitu cha kusikiliza na kuona raha, iwe ni kitu cha kukifata ili tupate kurehemewa na huyo ndio atakua aloishi maisha ya Dini, Amin

Saturday, December 1, 2012

MAHUJAJI WA DUNIANI PART-1

Asalaam Aleiykum,

Nini Hajj? Hajj ni Ibada maalum ilopangwa ili mtu afanye safari ya Kiroho(Sipiritual-Journey)kuhudhuria nyumba Takatifu(mji)uloridhiwa na kuchaguliwa na Mwenye-enzi-Mungu ili kukamilisha nguzo hii ya (Ibada).Likaregezwa shuruti la Ibada hii na kusemwa kwa Mwenye uwezo basi na akatende Ibada hii, Mletaji wa agizo hili anajua kuwa kuna wengine watakua hawana uwezo maskini, wengine wagonjwa nk.
Hiyo ni Hijja ya kwanza ambayo wengi tunaifahamu, Lakini kuna Hijja nyengine ambayo haina wepesi, ambayo haijaregezwa masharti, Hijja hiyo imelazimishwa kwa kila mmoja wetu na ndio imekua sababu yetu yakuja katika Ulimwengu huu ndani ya hijja hii nataka ujiulize maswali haya matano?
Mimi Nani?(1)Kwanini niko hapa Ulimwenguni?(2)Lini nitaondoka?(3)Wapi ninapokwenda?(4)Na Vipi yatakua mapokezi yangu huko niendako?(5).
Sote tumekuja katika Ardhi hii ya Mwenye-enzi-Mungu kama mahujaji ili tupate kutizamwa yupi katika sisi atotimiza Hijja yake hii ya Uhai na kurejea huko alikotoka akiwa safi. Ndio Maana swali la Mimi nani? linakuwa gumu, Mwanaadamu analiogopa kwani akijiuliza huwenda akakutana na ukweli, na ukweli siku zote unauma, ukweli unatisha, ukweli mzito na ndani ya ukweli  ni lazima utakua Muislam kamili, na ukiwa Muislam kamili ina maana lazima uitekeleze hiyo Hijja ya Uhai kama ilivokusudiwa na hijja yenyewe ni Ibada.
(1)Mimi Nani?
Mwanaadamu una vitu viwili ambavyo vinakufanya uwe Binaadamu, La kwanza ni Umbo lako ambalo linatokana na hii Ardhi, Umeumbwa kwa vizuri na Mollah wako baada ya kukamilika umbo hili hapo tena ukapewa kitu chengine kabisa nayo ni hiyo Roho. Kwa hiyo hapa tunaweza kusema wewe Mwanaadamu nusu nii hii Ardhi na nusu Nyengine ni hiyo Roho,(Lakini kumbuka huo ni mfano)Umbile la Binaadamu tunalifahamu lakini umbile la Roho hatulifahamu, Na hiyo Roho ni kitu chengine ambacho kinatoka kwa Mwenyewe Mwenye-enzi-Mungu na sisi hatuna elimu nayo, hiyo Roho ndio ilokuja kuhijji hapa ulimwenguni, kama anavosema Mwenye-enzi-Mungu katika Quraan Sura ya Sad aya ya 72.
"فَإِذَا سَوَّيۡتُهُ ۥ وَنَفَخۡتُ فِيهِ مِن رُّوحِى فَقَعُواْ لَهُ ۥ سَـٰجِدِينَ "
"Nitakapo mkamilisha na Kumpulizia Roho itokanayo na mimi, basi mwangukieni kwa kumsujudia."
Hiyo ndio Roho isiyokufa milele, wakati wa kufa kwako, kinachokufa ni kiwiliwili tu, Roho inashuhudia kifo chake na ukikamilika uchungu wa kutoka hiyo Roho, ikishakutoka inachukuliwa na kupelekwa katika makazi ya Barzak ambapo masafa yake ni makisio yenu maili 50,000.
"تَعۡرُجُ ٱلۡمَلَـٰٓٮِٕڪَةُ وَٱلرُّوحُ إِلَيۡهِ فِى يَوۡمٍ۬ كَانَ مِقۡدَارُهُ ۥ خَمۡسِينَ أَلۡفَ سَنَةٍ۬ "
Malaika na Roho hupanda kwake katika siku ambayo muda wake (Kwa makadirio yenu)ni Miaka hamsini elfu.
Hivyo ndivo ulivo mwanaadamu, hilo ndio jibu la mimi ni nani?
Kwanini niko hapa Ulimwenguni?Endelea part-2

MAHUJAJI WA DUNIANI PART-2

Asalaam Aleiykum,

(2)Kwanini niko hapa Ulimwenguni?
"مِنۡہَا خَلَقۡنَـٰكُمۡ وَفِيہَا نُعِيدُكُمۡ وَمِنۡہَا نُخۡرِجُكُمۡ تَارَةً أُخۡرَىٰ"
"Kutokana na hii (Ardhi) tumekuumbeni, na humo tutakurudisheni, na kutoka humo tutakutoeni mara nyengine tena,(Ili mupate kuishi tena)."
Uko hapa Ulimwenguni sababu kila kilichomo katika Ardhi hii pia na katika umbile lako kimo, Na baada ya mauti yako mwili wako unarejea tena kuwa Ardhi kwa mara nyengine tena, hiyo Ardhi unayo ikanyaga sasa hivi ukaifanyia ufisadi baadae na wewe watu wengine watakuja kukukanyaga mwili wako kama unavo kanyaga wewe sasa hivi."Ewe Mwanaadamu wewe na Mti hamna tafauti, jitizame wewe ni mbegu umetokea kuwa mwanaadamu na mti ni mbegu umetokezea kuwa mti, Ila tafauti yenu ipo katika hiyo zawadi Adhiim alo kukirim Mollah wako, akakutafautisha wewe na viumbe wengine akakupa kitu kitokacho kwake mwenyewe nayo ni hii Roho, Ngombe, paka na wengineo wanazo roho lakini si kama yako yako imepewa hadhi ya juu zaidi imetunukiwa fahamu mpaka ikatambua kama kuna kifo na mengineyo.
Amekuagiza Mollah wako yakua anakuleta hapa Ulimwenguni katika safari hii ya Hijja ya Uhai wako na ukishamaliza hakika utarejea kwake, Na hataki chochote kutoka kwako Mwanaadamu isipokua kumuabudu.
"وَمَا خَلَقۡتُ ٱلۡجِنَّ وَٱلۡإِنسَ إِلَّا لِيَعۡبُدُونِ"
"Sikuwaumba Majini na Binaadamu ila wapate kuniabudu"
Nipe Ahsante, Nishukuru na uridhike kwa hilo na yafate maamrisho yangu, zitizame alama za kuwepo kwangu, furahi kwa kujua hili jua, ule mwezi, zile nyota, hawa ndege,haya maua,  zitizame neema zangu hapa Ulimwenguni ili nipate kukuonesha zaidi utakaporejea kwangu.
(3)Lini Nitaondoka?
"وَمَن نُّعَمِّرۡهُ نُنَڪِّسۡهُ فِى ٱلۡخَلۡقِ‌ۖ أَفَلَا يَعۡقِلُونَ"
"Na tunayempa umri (mrefu), tunamrejesha nyuma katika umbo, basi hawayazingatii(haya)"
Tunakupa ishara za kuondoka kwako katika umbile lako, Unaanza baadhi ya mambo kukushinda, Tunakuondoshea uwezo wa kulala sana, Mapigo ya moyo yanapungua kasi yake, kiwango cha meno kinapungua mdomoni mwako, nguvu za macho zinapotea, mwendo wako unakua wa taratibu, Tunazibadilisha nywele zako na kuzifanya nyeupe, Tunakupunguzia marafiki unakua nao wachache, kasi yako ya kula inapungua unakua huwezi kula sana, Halafu mwisho tena mwili ulochoka unashukiwa na maradhi hapo tena unakua tayari kwa safari yako ya kurejea kwetu ulipotokea.
Wapi ninakwenda?Endelea part-3

MAHUJAJI WA DUNIANI PART-3

Asalaam Aleiykum,

(4)Wapi ninakwenda?
" إِنَّا نَحۡنُ نَرِثُ ٱلۡأَرۡضَ وَمَنۡ عَلَيۡہَا وَإِلَيۡنَا يُرۡجَعُونَ"
"Bila ya shaka sisi tutairithi ardhi na walio juu yake, Na kwetu watarejeshwa"
Unakwenda sehemu zinapokaa Roho, huko kuna walinzi wasomuasi  
Mollah wao, Ni sehemu ya upweke ni ngeni katika fahamu yako, jicho halijapata kuona, pahala ambapo hapana mfano wake na zaidi yategemea mizigo ulobeba na vipi hijja yako ya uhai uliitumia vipi, uliishi vipi na wenzio, ulikua ukisamehe, pahala unapokwenda inategemea na ulipotokea jee ulikua umeridhika? ulikua hutaki zaidi, ulikua hutumii nguvu kuchukua vitu vya watu, huko unapokwenda kuna daraja kwa hiyo mwenyewe ndio utajua unakwenda kukaa wapi magorofani au kwenye vibanda tena hayo utayajibu mwenyewe kutokana na vitendo vyako.
(5)Vipi yatakua mapokezi yangu?
Unataka kujua vipi yatakua mapokezi yako basi kwanza tazama nini matendo yako hapa kwenye Ulimwengu huu, Maneno ya Bwana Mtume s.a.w "anasema"Fanya wepesi mizigo yako unayochukua"kwa sababu safari unayokwenda ni refu, usije ukachukua magunia  ya dhanbi ukaja kuteseka milele, jionee huruma kwani wewe huwezi hapa duniani kubeba gunia moja vipi utaweza kubeba huko magunia japo mawili ya dhanbi.
Elewa hizi dhanbi unazotenda ni kitu kizito sana ndio maana utaona ili ipatikane mizani ifanane ukaambiwa ukija na jema moja tutakulipa mara kumi yake, kwanini? hebu sasa fanya hesabu zako utizame wewe mwenyewe inakuaje pale ukifanya dhanbi moja lina uzito wa kima gani(Mfano)tizama mfano huu wa kosa hili dogo, Umesema uongo  kuwa mwenzio kaiba ukamfukuzisha kazi, yatizame madhara yake.(1)Nyumbani familia yake hawana chakula(2)Mtoto wake kaumwa hana pesa za kumtibia mpaka kafa(3)Na yeye anampenda mwanae kalia mpaka kaumwa(4)sasa hawezi hata kutafuta kazi(5)anagombana na mkewe sababu haleti chakula(6)anakua omba omba huku na kule anaadhirika(7)watoto wake hawawezi kusoma tena(8)Ibadah hawezi kufanya tena hana utulivu wa ki akili(9)watu katika familia yake wanaanza kutafuta riziki kwa njia ya haramu(10)Magonvi yamezidi anaachana na mkewe. Hiyo ni dhanbi moja ndogo inazaa mlolongo wa mambo hayo yote, hii ndio dhanbi ndogo wewe uliyo isahau, hiyo ndio mizigo unayo ambiwa uifanye mepesi usije ukenda na magunia mazito mazito, Sasa kumbuka katika Hijja hii ya maisha ushafanya dhanbi ngapi zenye mlolongo kama huo.?Nini habari yako wewe usotaka kumuabudu Mollah wako.
Anaendelea Kusema Bwana Mtume s.a.w "Fanya (ukithirishe)uzidishe zawadi unazochukua huko"Unarejea nyumbani fanya hima sana mizigo yako ya (thawabu)zawadi hizo ziwe nyingi mno, punguza mizigo ya maasi ili upate kuzidisha magunia ya wema, Pia napenda uelewe wema haununuliwi dukani, thawabu ni kitu cha bure cha kuchuma na miti yake ni mingi na kila moja malipo yake ni mara kumi, kusaidia mayatima si kwa kuwapa chakula tu bali kuwachukua na kuwalea, kusaidia watu wasojiweza, kuwalisha maskini, kuwonea huruma walofikwa na matatizo ukawasaidia kuyatatua, kusomesha watu, kuwahudumia wagonjwa, kuwaenzi na kutunza familia yako, kufanya Ibadah kwa wingi vyote hivyo ni zawadi katika hijja hii ya Uhai, hata kukisadia kinyama pia katika zawadi, kumsaidia mtoto kuvuka barabara pia katika thawabu, ukimkamata mkono mtu mzima ukamsaidia pia moja katika zawadi Mwenye-enzi-Mungu atujaalie tuwe wenye kutekeleza sio wenye kusoma tukayaacha hapa hapa, Mollah tupe Imani na nguvu ili mazoezi yetu yawe katika kufata amri zako, tumiminie mapenzi yako na Rehma zako tuishi katka hali ya kukumbuka wewe Daima.Amin

Saturday, November 24, 2012

BALAA ZA UJANANI PART-1

Asalaam Aleiykum,

Nakushukuru Mollah wangu kwa kunipa siku nyengine ya Uhai nikaweza kukutukuza kwa zawadi hii Adhim, Nakushukuru Mollah wangu nimeamka nikiwa Hai naweza kuvuta pumzi, Naweza kutembea, Naweza kuijua Familia yangu na nikiwa mzima wa Afya.
Leo hii Mollah wangu ungetaka ningekuwepo kaburini kama walivyo tangulia walopita kabla yangu, Lakini kutokana na uweza wako bado hujanihitaji Mollah wangu, Na hayo yote si kwa mahitajio yangu mimi , Mimi sina amri kwa hilo, hichi ni kitu ulonikirimu wewe pasi mimi kuomba, Umenipa uhai huu kwa ridhaa yako na mapenzi yako juu yangu, Basi kwa hilo sina budi mimi ila ni kukushukuru na kukumbuka kila wakati Mollah wangu.
Leo tena umenipa fahamu na uwezo nitaweza kula na kunywa, Nitaweza kuwaona wanangu na wote walo wangu na marafiki zangu, Nitaweza kutoka na kurudi kwa salama nyumbani kwangu bila ya khofu yoyote ile. "Ewe Mollah wangu hakika umenipa Uhai huu wakati mimi sikua na thamani yoyote ya kupewa zawadi hii, Umenidiriki nivute pumzi hizi bila ya tabu wakati mimi nikiwa katika hali ya kukuasi Mollah wangu katika ujana wangu, Na unaendelea kunikirimu Neema hii hali naendelea kukuasi hata sasa katika uzee wangu lakini wewe upo katika hali ya kunipa nafasi labda leo au kesho nitakukumbuka Mollah wangu ili upate kunisamehe".Umenipa mimi furaha na afya wakati ule nilipo kukimbia nikawa sikukumbuki hata sekunde moja, yote hayo Mollah wangu umenisubiria, sasa sina mimi ila kujawa na shukurani katika moyo wangu na nimeridhia lolote lile litakalo nifika basi najua pengine ni mambo niliyofanya Ujanani ni makosa yangu mwenyewe ya kushindwa kujichunga wakati wa Ujana wangu ndio yalo nifikisha hapa nilipo.
Nikipata maumivu ya mwili au kero za Akili basi najua hili nimelisababisha kwa makosa yangu ya kupotea katika njia yako ya uongofu, Na mimi mwenye kukumbuka yale yote nilotenda katika Ujana wangu kama ulivosema katika kitabu chako kitukufu sura ya Qiyama aya ya 13" بَلِ ٱلۡإِنسَـٰنُ عَلَىٰ نَفۡسِهِۦ بَصِيرَةٌ۬ ""Bali mwanaadamu ni shahidi juu ya nafsi yake"
Nilikua mimi mchapaji wa mtindi (ulevi),Nilikua mimi sitoki vilabuni,Nilikua mbele ya hadhara ya watu nikipanda kwenye kiti nacheza viuno huku wengine wakinipigia makofi na wengine wakinitizama kwa matamanio sote tukitenda makosa lakini mimi ndio nilikua sababu ya kosa hilo.Nilikua nikivuta madawa ya kulevya, Nilikua nikiiba Serekalini na nikiona kama jambo la kawaida,Nilijiunga na vikundi vya uzinifu na kwangu ikawa kama jambo la kawaida, nilikua nadhulumu watu na kuwapiga nikisahau kabisa kuwepo kwako Mollah wangu, Najua yote hayo yapo hayajafutika na mengine naendelea kuyatenda sijui hali yangu itakuaje wakati utakapofika wa sasa wewe kunihitaji Mollah wangu ili nije kukutana na wewe. Na wewe utaniuliza kwani Mjumbe wangu hakusema lolote kuhusiana na Kadhia hii ya Ujana?-Endelea part-2

BALAA ZA UJANANI PART-2

Asalaam Aleiykum,

Anahadithia Ibn Abbas r.a"Kasema Bwana Mtume s.a.w""Kamilisha matano kabla hayajakufika matano"Yafanyie kazi matano hayo, kuwa makini katika mambo haya matano, jichunge sana katika kadhia hii ya mambo matano.(1)Ujana wako kabla haujakufika utu uzima,(2)Na Afya yako kabla Maradhi hayajakuvamia,(3)Utajiri wako kabla Hujafilisika,(4)Na Faragha yako kabla mambo hayaja kushughulisha,(5)Na Uhai wako kabla Mauti hayaja kuhudhuria.
Sasa hapo naya kusanya yote matano haya ili niweze kuyatia kwenye ukurasa mmoja ili upate kuyasoma kwa pamoja usije ukababaika.
Balaa za Ujana hazisemeki unaweza kuangua kilio ukikumbuka kuwa wewe ndie ulikua una andaa picknic na machupa ya ulevi, wewe ndie mwenye kuandaa ngoma za msondo na chakacha ili watu wapate kumsahau Mollah wao, wewe ndie mwenye kutembea umevaa (Backless)unaonesha watu mgongo wako. wewe ndie mwenye kuvaa kisuruali kifupi unaonesha watu mapaja yako, leo hayo yote yamepita umebaki wewe na sisi uko wapi ujana wako, Umepita kama moshi na yote ulotenda yamehifadhiwa halijafutwa hata moja, rekodi yako imetunzwa kwa umakini mkubwa na kama utabisha Viungo vitasema "Ewe kijana sisi ni mashahidi wako kwani hujaambiwa katika sura ya Yaasin aya ya 65.
" ٱلۡيَوۡمَ نَخۡتِمُ عَلَىٰٓ أَفۡوَٲهِهِمۡ وَتُكَلِّمُنَآ أَيۡدِيہِمۡ وَتَشۡہَدُ أَرۡجُلُهُم بِمَا كَانُواْ يَكۡسِبُونَ"
"Siku hiyo vitafungwa vinywa vyao, Itazungumza Mikono yao na itoe Ushahidi miguu yao kwa yale waliyokua wakiyachuma".
Ajihadhari Mwanaadamu siku ile viungo vitakapo kuwa tayari kumwaga siri zake, Vitaongea na kusema kweli mimi nilikua naishi maisha yangu kama Mcheza Cinema(Actor na Actress)Nilikua siwezi mimi kutoka katika nyumba yangu ila nijipambe, nitie piko, nitengeneze kucha,na Nywele niziachie nk, ndio nitoke, hivi hivi watu watanionaje na mimi nimeumbwa sijapendeza, Mimi nilikua nawaalika waja wako ili wanitizame mimi wapate kukuasi wewe na kukusahau Mollah wangu, hivyo ndivyo nilivoutumia Ujana wangu.(1)
Na Afya ulonipa nilikua nacheza mipira masaa mawili, Nakimbia riadha,nilikua na kula na kushiba mpaka nikawa nanyanyua vyuma nimejiunga (Gym)kwa uzima wa afya ulonipa, Lakini nyumba yako ya Ibada kwangu ilikua Marfuku, Ulikua ukiniona nikicheza pachanga (Disco)mpaka chini lakini nikiitwa kusujudu nilikua na kasirika sana hassa wakati wa Alfajiri.(2)
Na Uliponifungulia Utajiri Mollah wangu mtaa ulitingishika watu wote walijua mpaka paka wangu nilimvisha kengele, Niligeuka  mimi kuwa mcheza Senema maarufu nikiji fagharisha kwa kila aina ya starehe kuanzia ujenzi wa jumba la kifahari na magari yake sikujali chochote katika maagizo yako(3)Na Wakati ulo niruzuku ukanipa nafasi ya kuwa peke yangu ili nikukumbuke wewe, Hapo ndipo nilipotafuta (Whatsup)iko wapi, Computer iko wapi, Facebook iko wapi mchezo wangu kwenye TV utaanza saa ngapi, barazani kuna nini, hivyo ndio nilivokua natumia wakati wangu wa Faragha.(4)Na jambo la (5)ni kama ilivoanza mada kuelezea hali ya Uhai kabla ya Mauti.Basi leo uko wapi Ujana uliokua unaringia ulisahau maneno ya Mollah wako katika sura ya Yaasin aya ya 68
"وَمَن نُّعَمِّرۡهُ نُنَڪِّسۡهُ فِى ٱلۡخَلۡقِ‌ۖ أَفَلَا يَعۡقِلُونَ"
Na tunayempa Umri (mrefu)tunamrejesha nyuma katika umbo, basi jee hawayatii akilini(Kuzingatia).
Leo Ujana uko wapi huwezi hata kufanya mazoezi, Afya imekimbia umegubikwa na maradhi,Kipato sasa huwezi kukipata tena, kukaa peke yako sasa unaogopa, na pazia la Uhai lishafunikwa mgeni unae mtaraji Mauti yupo njiani, Basi yale Manne(4)umeyakosa hili lilobaki la Uhai bado unalo jitahidi katika hili kabla hujenda kukutana na Mollah wako.Zidisha Ibadah na Kuomba Maghfira Asaa Mollah wako huenda akakusamehe.

Abdulla Baja


Saturday, November 17, 2012

KIPIMO CHA IMANI-PART-1

Asalaam Aleiykum,

Hakuna jambo ambalo mwanaadamu anajihadaa kama kujinasib ana amini, ikisha ndani ya nafsi yake akawa anajua moyoni mwake hakuna hata chembe ya (Imani)Darsa yetu ya leo inagusa pahala penye uchokozi, tunakwenda kupachokoza pahala hapo ili upate kujua kumbe mimi siamini chochote, leo kamata kipimo chako ujue thamani ya Imani yako, halafu mwisho jiulize hivyo mimi naamini au nimejaa wasiwasi tu. 
Ili kukufanyia urahisi wakujua tafauti ya Mtu alokua hana Imani na Mwenye Imani nimekuchagulia visa hivi viwili ili vitufungulie darsa yetu ya leo, visome kwa umakini halafu utajiamulia mwenyewe ingekua wewe kundi lipi ungetamani kujiunga nalo. Hebu jikumbushe visa hivi viwili vimetokea katika miji tafauti, kimoja kimetokea katika mji wa (Lindi)ambapo walimaliza waumini kadhaa wakiislam kusali ikisha wakakaa Barazani, akatokea Mtu mmoja kashika panga mkononi akauliza ghafla jee hapa pana Muislam yoyote, waliopo pale barazani kwa khofu wakatingisha vichwa kuashiria hakuna Muislam huku kila mtu anatetemeka kwa khofu, yule Mtu akashika njia akenda zake, baada ya nusu saa akatokea kwa mbali huku panga lake limejaa damu anakuja haraka haraka, Barazani hakukaa mtu, walisema walokaa pale huyo yule jamaa sasa anarudi tumekwisha anarudi kuulizia kama kuna mkiristo miongoni mwetu, kumbe maskini yule Mtu alivouliza mwanzo alikua anataka akachinjiwe Ngombe wake kwa sheria za kiislam, na hii mara ya pili anarudi ili kuwaomba watu wakachukue sadaka ya nyama alipofika karibu kaikuta baraza nyeupe. Hizo ndizo zilivo Imani zetu, tukiulizwa una Amini tunatingisha vichwa kuashiria ndio, kumbe moyoni hapana kitu, Sala zote mtu anakwenda kusali kwa kuogopa moto tu, na wala si kwa ajili ya Mwenye-enzi-Mungu wake, hivyo ndio wengi Imani zetu zilivyo.
Na kisa cha Pili hiki kimetokea katika mji wa Basra kule Iraq, siku moja Darweish mmoja alikua ameketi (Zawiyyan)kwenye nyumba ya Ghorofa moja, alikua amezama katika hali ya (Wajid)kapotea kwa Mollah wake kwa ajili ya Ibadah, Darweish yule akawa anazungumza na Mollah wake "Anasema""Ewe Mollah wangu nijaribu mimi kwa chochote katika mitihani yako ili nipate kujipima mimi mapenzi yangu juu yako wewe, na mimi nafahamu mtihani wako unakuja kwa njia tafauti pasi kuwa na sababu yoyote,naomba mimi hilo ili nipate kuridhika, anamaliza kauli yake hiyo huku chini wanapita vijana na (Rika)zao wanaimba kasida hii""Kama kweli mpenzi wa Mungu chupa ujiunge nasi"(KAMA KWELI MPENZI WA MUNGU CHUPA UJIUNGE NASI)hawajamaliza mara ya tatu maneno haya mara wanamuona Darweish anazunguka na majuba hewani kutokea Ghorofani kajiachia, alipofika chini vijana wote wakakimbia Darweish huyo akakusanya majuba yake akarejea ndani ya nyumba yake bila ya kuumia hata kiungo kimoja.
Hiyo ndio Imani,. Sasa ikiwa leo na wewe mpenzi wa Mungu basi chupa ujiunge nami ili tupate kuzijua Imani zetu zikoje ili kama dhaifu tupate kuzifanyia kazi. Kumbuka katika safari hii hatakiwi mwanasiasa, au msomi, au mfanyabiashara au mpiga porojo  anotakiwa katika safari hii ni yule mpenzi wa Mungu mwenye kutaka kujua Imani yake, na huko upande wa pili kuna nini? na kwanini mimi simo kwenye kundi la wenye Imani?Endelea Part 2

KIPIMO CHA IMANI PART-2

Asalaam Aleiykum,

Nini Taqwa? Taqwa ni mapenzi, nini mapenzi, mapenzi ni njia au kivuli cha Imani, nini Imani, Imani ni msingi wa Ibadah, nini Ibadah, Ibadah ni njia au mwenendo wa kukutoa kwenye giza kwenda kwenye nuru, Kukuondoa kwenye hali ya kuto kuona kwenda kwenye kuona, Kukutoa kwenye Hamaki kwenda kwenye Huruma, Kukutoa kwenye kuadhibu kwenda kwenye kusamehe, kukutoa kwenye kusahau kwenda kwenye kukumbuka, kukutoa kwenye mazungumzo kwenda kwenye kusabihi, na mwisho kukutoa kwenye kiwiliwili kwenda kwenye Roho na hapo tena ni marejeo yetu sote kwa Mollah Muumbaji.
Sasa Ikiwa tushamaliza kuujua huo msingi hapo juu wacha tumalizie na nguzo zake ambazo sote tunazijua na kufahamu ziko sita, Katika nguzo hizi tumeambiwa tuziamini, lakini wengi katika sisi hakuna anazo ziamini ila tunazikubali, ni vizuri kukubali ndio mwanzo, lakini kinachotakiwi hapo ni kuziamini kwani kukubali tu wakati wowote unaweza kuzikataa (ndio maana wale walokaa barazani wakasema hakuna muislam hapa)ndio maana zikaitwa nguzo za Imani.Sasa chukua kipimo mwenyewe ujiulize ndani ya nafsi yako umeziamini au umezikubali ukipata jawabu ukajijua hujaamini umekubali tu Basi Nakwambia(Kama kweli mpenzi wa Mungu chupa ujiunge nami)ili utazame zaidi katika hizi Ishara ntakazo zitaja ili ujue ngapi unazo na hapo utajua kipimo cha Imani yako. Jiulize hivyo kweli mimi nina Imani?Nimeshawahi mara ngapi kuwalisha mayatima (1)Jee nimeshawahi kuwapa msaada wajane bila ya kuwatamani (2)Nini hali ya Muombaji pale anaponifata nimpe japo chakula natekeleza hilo (3)Nini hali ya Maskini jee nawafanya kuwa ndio marafiki zangu (4)Naweza kujizuia mimi nisiseme watu (5)Naweza kukaa siku mbili nisiseme uongo(6) nguzo sita namie nimetaja mambo sita lakini vipimo ni vingi sana vya hiyo Imani na kama mizani yako bado haijainuka hata kidogo kwa mambo hayo sita basi nakuomba "(Chupa ujiunge nami)"Ili tupate kuzikarabati hizo nguzo isije nyumba yako ikaporomoka kwa kukosa nguzo madhbuti.
Nguzo hizi zinafahamika uzuri kwa maandishi lakini kuna tabu kubwa kuziamini hususan kwa sisi viumbe wa kawaida ambao bado hatujaamua kuchupa, lakini kuna hii nguzo moja ambayo kidogo unaweza kujitahidi, sasa ni nguzo gani hiyo?ambayo ndio pekee inakugusa hiyo sehemu inapo kaa Imani, Nguzo yenyewe hii ya (kuamini vitabu vyake)hili la kitabu kuna wakati unachungulia ndani kutaka kujua kuna nini, angalau kidogo linakugusa pahali ukawa unakubali baadhi ya mambo, Na kama kitachomwa moto kitabu hichi unapata hasira japo kwa mbali na hamaki zinakushika, hapo angalau japo kidogo Kimizani chako kina nyanyuka, inaonesha unayo chembe ya mbegu ya Imani, Ndani ya chembe hiyo ndio mie nataka nitie mbolea ili upate kuota mti mkubwa wa Imani wenye matawi mingi.Sasa wacha tukamate nguzo hii ya kitab tutizame imesema nini na inathibitisha vipi hayo tuloyataja mwanzoni kuhusiana na kadhia hii ya Imani. Endelea-part 3

KIPIMO CHA IMANI PART-3

Asalaam Aleiykum,

"الٓمٓ (١) ذَٲلِكَ ٱلۡڪِتَـٰبُ لَا رَيۡبَ‌ۛ فِيهِ‌ۛ هُدً۬ى لِّلۡمُتَّقِينَ (٢) ٱلَّذِينَ يُؤۡمِنُونَ بِٱلۡغَيۡبِ وَيُقِيمُونَ ٱلصَّلَوٰةَ وَمِمَّا رَزَقۡنَـٰهُمۡ يُنفِقُونَ (٣) وَٱلَّذِينَ يُؤۡمِنُونَ بِمَآ أُنزِلَ إِلَيۡكَ وَمَآ أُنزِلَ مِن قَبۡلِكَ وَبِٱلۡأَخِرَةِ هُمۡ يُوقِنُونَ (٤) أُوْلَـٰٓٮِٕكَ عَلَىٰ هُدً۬ى مِّن رَّبِّهِمۡ‌ۖ وَأُوْلَـٰٓٮِٕكَ هُمُ ٱلۡمُفۡلِحُونَ ("٥
"Hiki ni kitab kisichokua na shaka ndani yake, ni uongozi kwa wanao mcha Mwenye-enzi-Mungu.Ambao huyaamini yasio onekana na kusimamisha sala na kutoa katika yale tulo waruzuku.Na ambao wanaamini yaliyoteremshwa kwako, na yaloteremshwa kabla yako na wanaimini (hiyo)Akhera.Hao wako juu ya uongozi utokao kwa Mollah wao, Na hao ndio wenye kuongoka."
"Aya hiyo ya pili imeanza kimaajabu"imesema hakika hichi ni kitabu ambacho hakina shaka ndani yake na ni muongozo(Kwa wapenzi)Wamchao Mungu,Maana yake kama utakifata kitab hichi (Quraan)basi ndani ya hiki kitab kuna muongozo na muongozo huu ni ule unao kukupeleka kwenye Imani, kwa hiyo ni vizuri kama unasimamisha Sala na kumpenda Mollah wako na Mtume wake basi umo katika (njia ya Uongofu)na ukikaa katika njia hii kuna siku utafunguliwa hiyo Imani.
"Aya ya tatu ikasema Ambao wanayaamini yasio onekana na kusimamisha sala na katika yale tunayo waruzuku wanayatoa"
Itabidi hapa mstahamili ili tupate kuchuma katika mti wa faida kuhusiana na hilo neno kuamini yasioonekana. Ina hadithiwa katika riwaya za hekima, kuna siku walikaa Mawalii wawili pamoja na wanafunzi wao, Ikawa walii mmoja anataka kumwambia mwenzie kitu lakini hawezi kufanya vile mbele ya wale wanafunzi, akaagiza aletewe karatasi nyeupe anataka kuandika kitu, wanafunzi wake wakamletea, akachukua kidole chake cha Shahada akawa anaandika kwenye ile karatasi alipomaliza akampa yule walii mwenzie yule walii aliikamata ile karatasi akaitizama kwa njia ya kusoma ikisha akaangua kicheko kikubwa, Walo hudhuria pale wakaona sasa mambo yamekua makubwa, ama walimu wagonjwa au kuna miujiza mikubwa imetendeka mbele yetu, wakashikilia sana wale wanafunzi kuwauliza walimu wao nini kilicho andikwa kwenye karatasi ile lakini hawakupata jawabu la swali lao, Baada ya muda kupita yule muandikaji wa ile barua mauti yaka muhitaji, yule mwenzie alobakia akawaita wale wanafunzi wote akawaambia leo nitakwambieni nini kilichoandikwa na mwenzangu siku ile, Alicho andika mwenzangu siku ile katika ile karatasi nyeupe na nyie mkawa hamuoni yale maandiko alisema maneno haya,"hawa wanafunzi wangu nimekaa nao sasa yapata miaka sita, hawanifahamu wala hawafahamu kitu, hawatizami dalili wala hawazioni, hawaelewi chochote ninacho wafundisha,utadhani macho yao yamepofuka au masikio kuzibwa, basi kama mauti yatanihitaji mimi mwanzo naomba uwape habari hii. Wale wanafunzi wakamuuliza vipi wewe uliweza kuisoma ile karatasi nyeupe isiyokua na maandishi, Akajibu kulikua hakuna miujiza wala makarama ila ilikua wakati anaandika anatumia ishara na alama za herufi kwa kidole chake na mimi nilikua naangalia kile kidole kinaandika herufi gani basi nikawa naunganisha neno, Na nyinyi wakati ule mlikua hamjui kuyatizama yasio onekana(yalo Ghaib).Na wewe ungekuwepo wakati ule ungebisha, ungeshangaa na kuamini makarama, lakini dunia yetu ya leo unamuona (Bubu na Kiziwi)wote wanazungumza kwa ishara na alama.Haya ndio matatizo yetu makubwa hatujui kutizama ishara zote Mollah wetu alotuwekea, sasa ikiwa umejipima na kujigundua bado Imani yako ni dhaifu jaribu kuangalia Ishara na Alama za Mollah wako asaa mizani yako ya Imani itapanda juu, pengine utafunguliwa kuona mambo ili izidi Imani yako na imani ikiingia sawa sawa basi halitoki tena jambo hilo la Imani mpaka mwisho wa Umri wako na utakua unaamini kama unavo liamini jua na mwezi kuwa vipo na hayo mengine utaamini hivyo hivyo, na ikisha kuingia Imani hiyo kwako kila wakati utakua wakati wa "(kusimamisha hiyo Sala)" na kama mtu atakutania tu, "kama kweli mpenzi wa Mungu chupa ujiunge nami"hapo hapo husiti au kusubiri chochote kile, sijui nyumba nitamwachia nani, gari atachukua nani, pesa za bank itakuaje, hufikiri mambo hayo kabisa ila unajiachia kama yule Darweish.Endelea part 4

KIPIMO CHA IMANI PART-4

Asalaam Aleiykum,

Na hapo tena  kila unacho Ruzukiwa unafanya haraka haraka kukitoa, na kumbuka kila ukitoa kwa njia ya Imani basi huku unazidishiwa kupewa ili upate kutoa tena. 
Na hao ndio walo amini yaloteremshwa kwako "Ewe Mjumbe wa Mwenye-enzi-Mungu" na yaliyo teremshwa kabla yako, yepi hayo walo yaamini ikawa ndio nguzo zao. Dalili ya nyumba, maana yake kuna mtu anaishi, Ukiona na kuutizama Ulimwengu basi una hakika yupo alouumba naye huyo Mollah wako(1)Dalili ya Hukumu ni haya matendo ya Dhanbi na Thawabu kwa hivyo ni kuamini hiyo Akhera na siku ya (Hukumu)Kiyama.(2)Kuupata huu ujumbe wa Mwenye-enzi-Mungu na ushaidi uliopo wa macho kwa kujionea na mabaki yalobakia katika historia ni kuamini Mitume yake.(3)Kuyapata maneno kama haya yenye uthibitisho na maliwazo na ukumbusho pamoja na maonyo ni kuamini Vitabu vyake.(4)Kukubali maneno ya Mollah wako na kujua kwamba utakufa na Roho yako itachukuliwa ni kuamini Malaika wake.(5)Kujua kwamba vyote viliyomo mbinguni, nyota, mwezi,jua na viliomo ardhini miti, majani, wanyama, ukiwemo na wewe mwanaadamu nyote mmekamatana ni kitu kimoja basi hiyo ndio njia ya kuamini kheri na shari vyote vinatokana na yeye Mollah wako.(6). Na huo ndio muongozo utokao kwa Mollah wako na anayepata muongozo huu unampeleka katika Imani kubwa na anakua ni mwenye kufanikiwa ndipo akiambiwa chupa kwa ajili ya Mwenye-enzi-Mungu hasubiri hata itamkwe tena ila anakua kesha hudhuria kwa Mollah wake bila ya kuchelewa.
Ukitaka kuijua Imani yako patafute wapi yanatokea machozi, wapi zinapotokea hasira,wapi inapotokea chuki, wapi zinapotokea huzuni, wapi zinapotokea huruma, wapi zinapotokea hisia ukisha pagundua hapo pahala basi subiri hapo hapo wala usichoke asubuhi na usiku wala usifanye chochote baada ya muda Mollah anajua kama kweli wewe mpenzi wake na yeye ndio atakufungulia huo mlango wa Imani, na ukiipata hiyo Imani wewe unakua hakika Miongoni mwa waloongoka.
" قَالَتِ ٱلۡأَعۡرَابُ ءَامَنَّا‌ۖ قُل لَّمۡ تُؤۡمِنُواْ وَلَـٰكِن قُولُوٓاْ أَسۡلَمۡنَا وَلَمَّا يَدۡخُلِ ٱلۡإِيمَـٰنُ فِى قُلُوبِكُمۡ‌ۖ وَإِن تُطِيعُواْ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُ ۥ لَا يَلِتۡكُم مِّنۡ أَعۡمَـٰلِكُمۡ شَيۡـًٔا‌ۚ إِنَّ ٱللَّهَ غَفُورٌ۬ رَّحِيمٌ "
"Walisema Waarabu (wanaoishi majangwani)Tumeamini(Wanamwambia Mtume s.a.w)sema hamjaamini, lakini semeni tumesilimu, Maana Imani haijaingia katika mioyo yenu, Na mkimtii Mwenye-enzi-Mungu na Mtume wake, hata kupunguzieni chochote katika vitendo vyenu, Hakika Mwenye-enzi-Mungu ni mwingi wa kusamehe na Mwingi wa Kurehemu. Namalizia kwa Aya hii ili upate kujijua na kuongeza juhudi na "KAMA KWELI MPENZI WA MUNGU BASI CHUPA UANZE LEO HII KUITAFUTA NA KUIJAZA HIYO IMANI"na Mollah wako atakusaidia kwa hilo Inshaallah.

Abdulla Baja


Saturday, November 10, 2012

NANI KAMA MAMA?PART-1

Asalaam Aleiykum,

Leo wacha nikuchukue tuingie katika Dunia ya Mama, Kwanini nikasema tunaingia, nimesema tunaingia kwa sababu dunia ya mama ni ulimwengu wa ajabu, na wanaadamu desturi zetu ukishazaliwa, ukalelewa kwa mapenzi basi unakuwa huna haja ya kutizama nyuma au kwa maana nyengine hutaki kujua mahusiano yako na wazee hawa wawili. Zawadi hii adhimu hutaki kuijua, ila unaicha iendelee (Automatic), na hiyo (automatic)huenda ikafikia pahala inaharibika, inakua haifanyi kazi tena na hapo ndipo mahusiano yako na wazee wako wawili yanaanza kutetereka.
Sasa ikifikia hali kama hiyo ndio inatubidi tutembelee tena ndani ya Quraan-aya-ya-14-Luqman, ipate kutukumbusha,
"وَوَصَّيۡنَا ٱلۡإِنسَـٰنَ بِوَٲلِدَيۡهِ حَمَلَتۡهُ أُمُّهُ ۥ وَهۡنًا عَلَىٰ وَهۡنٍ۬ وَفِصَـٰلُهُ ۥ فِى عَامَيۡنِ أَنِ ٱشۡڪُرۡ لِى وَلِوَٲلِدَيۡكَ إِلَىَّ ٱلۡمَصِيرُ "
"Tumemuusia Mwanaadamu(Kuhusiana na kuwafanyia wema)Wazazi wako, Mama amechukua mimba(yako)kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha kunyonya baada ya miaka miwili,(basi)Nishukuru mimi na wazazi wako,ni kwangu mimi marejeo yenu"
Nilipoanza hapo juu nilitaja neno (Automatic)kusudio langu ni kueleza huo wasia ambao umo ndani ya jinsi(Being)yako, imeshaumbiwa ufahamu huu wa kuwafanyia wema wazee wao kama kuishi nao kwa uzuri na mapenzi, hii kwa wazee wako inakuja (Automatic)sio kwamba anakuja mtu kukuweka chini na kuanza kukupa wasia, ikiwa mtu atafanya hivyo elewa hizo ni taratibu zake au uzoefu wake, lakini wasia kutoka kwa Mollah wako unatokea ndani ya (Roho)yako ndio maana utajiona unawaonea huruma, imani, nk. Lakini aya imekwenda mbele ikakumbusha nishukuru mimi (Mollah)wako ikisha na wazee wako wawili, Hapa ndipo nikasema hebu tutizame nyuma, tuingie katika hii dunia ya Mama vipi kachukua mimba kwa udhaifu juu ya udhaifu, ukisha kuyajua hayo hapo pengine shukurani yako ya dhati itatokea moyoni.
Ili shukurani hiyo ikuporomoshe kwa maneno na vitendo, isije ukawa unaitoa shukurani hiyo huku umeshika kiuno huku unamtuma mama yako akuletee maji ya kunywa.
Nani kama Mama?
"Alikuja Mtu siku moja kwa Bwana Mtume s.a.w akamuuliza"Ewe Mjumbe wa Mwenye-enzi-Mungu, Nani Katika wanaadamu anastahiki awe kipenzi changu,(Nimfanye kuwa rafiki yangu)nimfanyie ihsani nimpe na mapenzi?Akajibu Bwana Mtume s.a.w "Mama yako,yule mtu akasema ikisha, Bwana Mtume s.a.w akasema tena Mama yako,yule mtu akasema halafu,Bwana Mtume akamwambia Mama yako, na Mara ya Nne akamwambia Baba yako.Hasemi Bwana Mtume s.a.w Ila maneno yake ni uthibitisho utokao kwa Muumba mwenyewe wa hao wanaadamu, Sasa kwanini     
Bwana Mtume s.a.w akasisitiza hususan Mama, ili upate kujua Endelea part-2

NANI KAMA MAMA?PART-2

Asalaam Aleiykum,

Uhusiano wako  na mama yako mpaka leo unabaki miujiza ambayo hatuwezi kutambua undani wake, kwanza kabisa huyu Mama akizaliwa tu anakuja na mayai yake kamili ndani ya tumbo lake, na katika mayai hayo moja wapo ndio hilo lilo kuzaa wewe, jee mapito yako kwa mama huyu ni bahati au kitu kilichopangwa?Kaa ufikiri kadhia hii halafu ujue kwanini ikatokea hivyo, mtizame Mama yako kwa jicho la huruma ujue kutokana na kudra ya Mwenye-enzi-Mungu yeye karidhia sababu ya uhai wako ianzie kwenye kiwili wili chake, yuko tayari achukue machungu yote na taabu zote ili na wewe upate ladha hii ya maisha ya kidunia.
Na muujiza mwengine ambao unadumu mpaka ya wawili nyie kuondoka katika Ulimwengu huu ni ule unao anzia tumboni katika kiunganishi chako wewe na Mama yako yaani kwenye (kitovu)Hapo katika miezi yote tisa yakuumbwa kwako ndio unapata huduma ya uhai wako, zinapita hapo (Electric-Transfer)baina yako na mama yako, ikawa aanchokila na wewe unapata faida zake, akihema kwa kupokea nguvu za uhai na wewe unapata kuishi(Umo tumboni umelala masaa ishirini na nne)kila kitu unafanyiwa, nje kukitokea msuko suko na wewe unashtuka mule ndani, kila kitu kimeambatana na Mama yako huku wewe umetulia unaendelea kuumbwa, na kila hatua ya kuumbwa kwako basi matatizo,magonjwa na shida zote zinamfika Mzazi wako huku yeye anastahamili na kumuomba Mwenye-enzi-Mungu "Ewe Mollah wangu nijaalie nikitoe kiumbe hichi kwa salama, hayo ndio maombezi ya Mama kwa mwanae ambae hata hajamuona au hamjui atakua kiumbe wa aina gani?.
Mapenzi ya Mama yanaanzia ungali tumboni, na inapotimia miezi tisa unazaliwa na kitu cha mwanzo kinofanyika unapewa uhuru wako ili uweze kuishi mwenyewe unakatwa ile(Life-support)Kitovu ,ile kamba ya uhai ikisha katwa baina yako na Mama yako sio mwisho wa wewe kumuhitaji Mzazi wako, ila baada ya muda mfupi tu una muhitaji huyu Mama aendelee kukupa huduma hii ya Uhai ili upate kuishi, hapo tena mahusiano ya tumboni yamekatika yanaanza ya kwenye (Kifua)kunyonyeshwa.Unaendelea kuwa muhitaji, unaendelea kumtegemea Mama takriban kwa miaka miwili au karibu na hapo, Na kama Mama atakua katili au hana huruma au ujana unamtesa akakudhulumu kukunyonyesha katika kipindi hichi basi maisha yako yote yatakua na matatizo ya hapa na pale kuhusiana na mapenzi au mahusiano yako na watu wengine.
Lakini Mama mwema ni yule apendaye kumnyonyesha mwanae na huku akimuombea Taufik kwa Mollah wake,Mjaalie mwanangu akue bila ya matatizo mpe afya njema na lau kama Mama huyu ataulizwa ghafla baina yako na mwanao nani unataka afe mwanzo, basi bila ya kusita au kujishauri atasema bora afe yeye ili huyu mtoto abaki.
Nani kama Mama? Huyu ndie leo wewe mtoto eti unaomba atakufa lini, mbona anateseka na anakutesa na wewe.Huyu ndie Mama mwenye kupokea machungu yote unayomletea au yanayokupata, huyu ndie mama mwenye kukupa mapenzi bila ya masharti yoyote.Huyu ndie Mama mwenye kusamehe kabla hata hujaomba hiyo samahani, Wallahi hakuna shaka ya mapenzi yako isipokua mfano wa miujiza,Hata watu wote wakikuchukia yeye anabakia kukupenda,yuko radhi akae na njaa ili upate kula wewe,yuko tayari akae macho ili wewe upate kulala,"wewe Mama mimi nikiumwa wewe unahangaika usiku kucha huku watu wote wamelala", uko radhi uteseke ili mimi nifurahi, wewe ndie unaenijua naumwa nini wakati hata siwezi kujieleza,Na sifa yako nyengine halipungui penzi lako hata tukiwa kumi unatupenda sote katika hali ilo sawa.
Nani kama Mama?endelea part-3

NANI KAMA MAMA?PART-3

Asalaam Aleiykum,

Mama ni wewe mpaka nikiwa mtu mzima mapenzi yako yanaendelea kama yalivo mwanzo, Leo hii nimekua mkubwa ukaja kuniozesha sasa niko na mke wangu au mume wangu eti nakukejeli mbele yake, Mimi nakupuuza na huku namuamini mume wangu au mke wangu na kukukadhibisha wewe, Mimi nina hali gani kama ghafla nitahudhuria kwa yule aloniumba. Leo imefikia eti nakutuma unikoshee vyombo, au uende dukani, na hivi ndivo jeuri ziliponifikisha.Nimefikia hali nayapuuza Maneno ya Bwana Mtume s.a.w alosema "Hakika ya hiyo pepo ipo chini ya nyayo za Mama zenu",Kwanini Bwana Mtume s.a.w akasema maneno haya na nini alikua anakusudia,"Kusudio hapo lilikua kukufahamisha ni lazima ujitupe, urejee katika hali ya chini kabisa mbele ya Mama yako, sio wewe umtume maji ya kunawa mkono Mama yako,ila unatakiwa wewe ukachukue hayo maji umnawishe Mama yako halafu usimame mpaka amalize kula hiyo ndio heshima na huko ndio kunyenyekea kwa mzee wako, wangapi katika sisi leo tunatenda hayo, leo akikuomba pesa ya kula  tu majibu yanayokutoka mpaka Malaika wanaogopa. Leo unasahau kama Mama yako alikua akienda msitu na nyika ili atie tonge kinywani mwako, yeye ndio kila akikaa anakuombea dua kwa siri na dhahir ili ufanikiwe.
Nani kama Mama?
Sasa kama unayatilia wasiwasi Maneno hayo ya Bwana Mtume s.a.w "Basi jikumbushe kisa cha kijana Alqamah"Yeye alikua  ni mwenye kujitahidi kufanya mambo mengi ya Ibadah, alikua akisimamisha Salah, (kipindi hakimpiti)akifunga sana(Saum ni kawaida yake)na katika mambo ya kutoa sadaka yeye alikua mbele sana katika kutoa, Yakaja kumpata maradhi na maradhi yale yakawa yanazidi, akamtuma mkewe akampe habari Bwana Mtume s.a.w"Akenda yule Mke kwa Bwana Mtume s.a.w "Akamwambia mume wangu Alqamah anaumwa Taabani Yaa Rasullallah"kanambia nije kukufahamisha. Bwana Mtume s.a.w akatuma Masahaba zake akiwemo Syd Bilal r.a wende nyumbani kwa Alqamah mkamtoleshe Shahada, wakenda Masahaba  wakamkuta Alqamah makhtuti, wakamwambia "Ewe Alqamah sema"(Laaillah-illa-Allah)Lakini ulimi wa Alqamah haukuweza kutamka, wakarejea kumpa habari Bwana Mtume s.a.w na akasema jee wazee wake Alqamah wa hai, akajibiwa Mama yake yupo hai lakini ni mtu mzima sana, akamtuma mtu akamwambie mama yake Alqamah kama ataweza kutembea na kuja kwa Bwana Mtume s.a.w laa kama hawezi basi Bwana  Mtume s.a.w atakwenda yeye.
Akainuka Mama yake Alqamah na fimbo yake akenda kwa Mtume s.a.w akamsalimia na Bwana Mtume s.a.w akarudisha salam ikisha akamwambia "Ewe Mama wa Alqamah niambie ukweli na kama ukidanganya basi utakuja wahyi kutoka kwa Mwenye-enzi-Mungu" ilikuaje hali ya Mwanao Alqamah(wakati yuko mzima)Akajibu Mama yake Alqamah alikua mwenye kusali sana, na akifunga sana, na akitoa sadaka sana, Akamuuliza tena Bwana Mtume s.a.w jee yalikua vipi mahusiano yako na mwanao Alqamah, yule mama akasema "Ewe Mjumbe wa Mwenye-enzi-Mungu, Hakika mimi nimefungika moyo wangu juu ya mwanangu"kwani alikua akimsikiliza Mkewe na akiniasi mimi(akinikadhibisha)Akasema Bwana Mtume s.a.w kufungika kwa Mama yake Alqamah ndio sababu mwanae hawezi kutoa Shahada, ikisha akamwambia Ewe Bilal r.a kanitafutie kuni(Mbao)ili apate kuchomwa moto Alqamah, Akasema Mama wa Alqamah hauwezi kuchukua moyo wangu kuona mwanangu anateseka, Akasema Bwana Mtume s.a.w adhabu ya Mwenye-enzi-Mungu ni kali kuliko hiyo na ni ya kuendelea, basi kama utataka asamehewe na Mollah wake itabidi Uridhie moyo wako na kama hukuridhia moyo wako hazitomfaa, sala zake wala funga zake wala utowaji wake wa sadaka midamu moyo wako umefungika juu yake.
Akasema Mama yake Alqamah Mwenye-enzi-Mungu ananishuhudia na Malaika wake na waislam wote walohudhuria hapa yakuwa mimi niko Radhi na mwanangu, Akasema Bwana Mtume s.a.w Ewe Bilal r.a nenda kamtizame Alqamah anaweza kusema (Laa-illah-illa-Allah)au hawezi, isije ikawa Mama yake Alqamah kasema kitu hakimo ndani ya moyo wake ila kanionea haya mimi, Akenda Bilal r.a akamsikia Alqamah anasema (Laa-illah-illa-Allah)akaingia ndani ya nyumba Bilal r.a na kuwaambia waliomo ndani kufungika kwa Mama yake Alqamah ndio kuliko fanya uzito wa kushindwa ulimi wa Alqamah kutamka shahada, mpaka aliporidhia mama yake ndio ulimi ukatamka na ukawa mwepesi, ikisha baada ya hapo Alqamah akafa siku ile ile.Sasa ikiwa Shahada imeshindikana nini habari ya kuipata hiyo pepo inakuaje? Endelea part-4

NANI KAMA MAMA?PART-4

Asalaam Aleiykum,

Nani kama Mama?
Leo unataraji pepo huku unamtuma mama yako akuletee chai, huku unapita ukisema anamkera mkeo au mumeo, Mama akiomba pesa ya chakula unamjibu huna wakati ukitoka unakwenda kuchapa matumizi kwa mambo ya kijinga, Nyie watoto wa kike haijambo kidogo mnajitahidi kuwafanyia hisani Mama zenu ila zidisheni unyenyekevu, Enyi watoto wa kiume nyie tahadharini sana na kuwatupa mama zenu na kuwasahau, yanakufikeni madhara na fimbo ya Mwenye-enzi-Mungu inakupigeni pasi na nyinyi kujijua, Unapita kujiuliza mbona mambo hayendi, mbona sina furaha, mbona nyumba yangu haikaliki kuna nini? mbona watoto hawanisikilizi, mbona kipato changu hakitoshi, kumbe hujijui umo katika kukanusha Maneno ya Mwenye-enzi-Mungu"Ni shukuru mimi na wazazi wako wawili"huyo ndio Mama ambaye leo umemtupa, leo humtizami, huwezi hata kumtembelea una harakati nyingi. Ewe mtoto umeambiwa muhudumie mama yako unasema huna uwezo eti unamajukumu mengi, nini habari yako wewe kama ghafla utafunga kauli huwezi kusema tena, Angalau mwenzio Alqamah alipata bahati Mama yake akamridhia, sasa nini hali yako wewe kama Mama yako akikutangulia bila ya kupata Radhi zake.
Sasa nini ufanye? vipi utamshukuru Mzee wako, itabidi tukitembelee kisa cha Nabii Mussa a.s "alipomuuliza Mollah wake nani atakua Rafiki yangu peponi?"Mwenye-enzi-Mungu akamwambia nenda katika njia mtu wa mwanzo utayekutana naye huyo ndie atayekua Rafiki yako peponi, Akatoka yule Msemezwa na Mollah wake Nabii Mussa a.s akenda kwenye hiyo njia akakutana na huyo mtu akamwambia leo nataka nikufate niwe na wewe kutwa nzima, yule mtu akamjibu sawa, wakatoka wakenda sokoni akanunua chakula wakarudi nyumbani walipofika walimkuta  
Bibi mtu mzima kakaa pembeni, yule kijana akatoa vile vitu akaanza kupika alipomaliza akachukua maji akamnawisha yule bibi halafu akaanza kumlisha ikisha akampa maji na kumrudisha kwenye kitanda, huku wakati wote Nabii Mussa a.s anamuangalia alipomaliza, Nabii Mussa a.s akamuuliza huyu bibi ni nani kwako, yule mtu akamjibu huyu ni Mama yangu, Nabii Mussa a.s akasema nilikua nakuona kila unachomfanyia huyu bibi unasema maneno, ni maneno gani ulokua unasema, akajibu kila nilipokua namfanyia kitu Mama yangu nilikua nikiomba Ewe Mollah nijaalie mimi kuwa Rafiki yangu Nabii Mussa a.s huko peponi. 
Nani kama Mama?
Huyo ndio Mama na hayo ndio malipo yake, hiyo ndio maana ya hiyo pepo ipo chini za nyayo za Mama zenu, "Ni Shukuru mimi na wazazi wako wawili"Kushukuru wazazi ni kuwatendea wema, kuwadekeza, kuwapa mapenzi, kusema nao kwa upole, usiwatolee jeuri, uwatizame kwa hali na mali, ukimuona anafanya kazi kuwa wa mwanzo kumsaidia, fanya kila uwezalo mpaka mama yako afurahi moyoni na akifurahi basi utaona matatizo yote yanaondoka utaipata furaha ya Raha mustarehe kama ulivokua tumboni nakukumbusha (Connection)bado ipo inaendelea mpaka mwisho wa Uhai wenu, na katika kiungo hichi ndipo inapokaa hiyo Radhi basi fanya jitihada usije ukaikosa au kuikata, Mwenye-enzi-Mungu wape Rehma zako za Usamehevu kwa wale wazee wetu walotangulia, wape afya njema kwa wale walobakia, na uwape umri mrefu wenye manufaa ya kukumbuka wewe daima-Amin

Abdulla Baja

Thursday, November 1, 2012

SHAIRI LA MCHA MUNGU-PART-1

Asalaam Aleiykum.

furaha ilioje ukipata nafasi ya kuyasikia maneno ya Mcha Mungu hasa wakati kama huu umemaliza siku za furaha za Eid-Adh haa, Anasema nini Mcha Mungu.
"Nilipojua kwamba katika Moyo wangu kuna uwezekano wa kukaa asiye kuwa wewe Mollah wangu, Basi nilifanya mimi jitihada na mashindano makubwa ili kuhakikisha kuwa haingii akakaa mwengine yoyote asiye kuwa wewe Mollah wangu, niliendelea mimi kuujaza Moyo wangu uongofu wa kila jambo utokao kwako hata ikawa haikubakia nafasi yoyote ya kukaa asiye kuwa wewe Mollah wangu".
Anasema Mcha Mungu nilipojua au nilipogundua au uliponijia mimi (Uamsho) katika moyo wangu kwamba kuna uwezekano wa kukaa asiye kuwa wewe, hapo nilianza kufanya jitihada kubwa nilishindana sana kwa ajili yako Mollah wangu ili asije kuingia yoyote yule Moyoni mwangu, Katika maneno haya kuna siri kubwa Mcha Mungu anataka kutupa na sisi faida ili tupate huo (Uamsho)litutoke lepe lepe la usingizi ili tusikubali tena kumpisha kila ajae kukaa katika Mioyo yetu.
Nini maana ya neno Uamsho?
Katika matumizi ya lugha ya Wacha Mungu neno hili kama mengine yote yana maana mbili, Maana ya kwanza ni ile inotumika katika sauti za kila leo kama vile ukiambiwa Uamsho, wewe utafasiri kwa maana nyingi tu unavopenda, labda umelala umekuja kuamshwa, Pengine unaamshwa ukale daku mwezi wa Ramadhan, au tafsiri nyengine kuwa kuna watu washaamka na sasa wanakuamsha na wewe pengine unadhulumiwa au unatawaliwa na shetani wanakuzindua, sasa basi tena kutawaliwa simama  udai haki yako, wote huo unaweza kuita Uamsho, hiyo ni maana ya nje ya Uamsho. Ama katika maana ya ndani ya Uamsho inakua kama alivoitaja Mcha Mungu nilipojua (Awaken) vipi inakua muamko huu? Mfano utaupata katika usingizi wako wa kawaida, hebu jichunguze vipi inakua pale mwanzo ukiamka asubuhi, jitahidi usifungue macho utaona kitu cha mwanzo kinacho kujia ni (Awareness)kujijua mie nishaamka hapo hujijui mie fulani babaake fulani au mie fulani mke wa fulani, habari hizo hufatia baadae.
Kitu cha mwanzo kukushukia ni elimu ya kujijua mie ni macho na hapo Mcha Mungu husema (Alhamdullillah)ukitulia katika hali hiyo ndio utagundua kumbe kuamka ni (Process)kama vile inavoingia Alfajiri au Magharib, ndio Mcha Mungu akasema "(Nilipogundua kumbe katika moyo wangu anaweza kukaa asiye kuwa wewe)"na ukitaka kujua vipi anakaa asiye kuwa wewe basi ukiliacha lile sharti la usifungue macho, ukaja ukayafungua hapo utaanza kuona mtiririko wa asiye kuwa yeye unavo miminika, zinaanza kuingia (Information)zote unasahau hata kama ulikua umelala, unaanza kukumbuka viporo vyote ulobakisha jana, basi kabla hujaamia katika hizo kumbukumbu kitu cha mwanzo kinacho kujia ni hiyo elimu ya kujua, na huo ndio Uamsho, ambao watu wengine wanautilia mkazo tu ili usije ukalala tena au ukaja kulazwa, sasa ufanye nini endelea part 2 ujue taaluma hii ya uamsho inaishia wapi.

SHAIRI LA MCHA MUNGU-PART-2

Asalaam Aleiykum,

Uamsho huu wa ndani au wa aina ya pili unatokana na Mollah wako, na Mtu au watu wakisha amshwa na Mollah wao inakua tabu tena kuwalaza hata ukitumia nguvu ukali hawalali tena, sababu wanakua washajua na siri ya kujua inakaa moyoni, ndio maana Mcha Mungu akautaja Moyo, na hakitajwi kitu chenye uzito kama moyo kikawa kitu cha upuuzi, lazima kuna faida kubwa kwa watakao kujua. Kwa fahamu zetu za haraka haraka tunafahamishwa moyo ni (Pump)inayo sukuma damu, ikisha tunaishia hapo hatutaki kwenda zaidi tukajua jee Moyo una siri gani kwetu sisi wanaadamu?.
Yapo mambo mengi yano pitikana katika Moyo ambayo wengi wetu hatuna habari nayo, Mcha Mungu aliposema "nilipogundua katika Moyo wangu anaweza kukaa asiye kuwa wewe" Haya ni maneno yalobeba siri kubwa ndani yake, na siri hii ina anza wiki tatu tu unapoanza kuumbwa katika(Umbo la kuonekana)mimba ikingia baada ya wiki tatu mpaka tano mapigo ya chombo hichi tayari yameshaanza kusikika na ambayo yataendelea mpaka mwisho wa umri(maisha)yako.
Kwa mtazamo wa nje moyo ni (Pump)inayosukuma damu, lakini kwa mtazamo wa Mcha Mungu anajua kuwa Moyo una kazi nyengine lakini mpaka uzinduke au upate(Uamsho)ndio unakutana  na hiyo siri ya utendaji wa kazi nyengine, na ukigundua siri hiyo ndio unakua, umefanikiwa, ushavuka na daima unakua Mcha Mungu lakini lazima siri hii akufunulie pazia Mollah mwenyewe na hapo inakua tabu tena kwa wewe kurejea katika ulimwengu wa maasi, shida za kidunia. Inakuaje chombo hichi chenye kudumu na sisi mpaka mwisho wa uhai wetu na hizo kazi za siri? Na siri gani alogundua Mcha Mungu hata akautaja Moyo?Wanasema wanasayansi kitu cha mwanzo kufanya kazi katika huo Moyo kinaitwa(Sino-Node)au(Electric-Conduction-System)huo ndio Moyo kitaaluma tunaishia hapo (Pump)inafanya kazi.
Lakini Mcha Mungu kakataa kuishia hapo, kaamua kwenda mbele zaidi kidogo ndio (akagundua kwenye moyo kuna nafasi ikiwa hakua makini nafasi hiyo yaweza kukaliwa na asiye kuwa Mollah wake, kuna wengine watashangaa mbona sasa anazungumza mambo mapya, mbona haya mageni, vipi moyo ukawa na kazi nyengine, naam hiyo ni kawaida walishangaa wenye kushangaa pale walipoambiwa maji ni (Gas)mbili na (formula)yake ni (HO2)lakini mshangao unakuja hapa, Mbona gas hizi mbili zipo lakini hazigeuki maji, Siri yake lazima ipatikane kitu cha tatu nayo hiyo (Elecricity)ndio kifanye hayo maji, Mcha Mungu yeye kaita (Rehma)Quraan-Anbiya-"وَجَعَلۡنَا مِنَ ٱلۡمَآءِ كُلَّ شَىۡءٍ حَىٍّ‌ۖ أَفَلَا يُؤۡمِنُونَ "
"Tukajaalia maji (Kwa)kila kilicho hai(Tulichokiumba), Jee hawaamini".
Naam hiyo iliyomo kwenye Moyo na kwenye maji lazima ipatikane sasa mnaulizwa jee hamuamini?, Kuwa mstahamilivu tuko tunamfata Mcha Mungu na maneno yake, usije ukahadaika na maneno ya Mcha Mungu ukaja kukwama kwenye maneno, bali chukua ujumbe uliomo kwenye maneno haya,"Nilipogundua katika huu Moyo wangu kwamba anaweza kukaa asiye kuwa wewe"jee unataka kujua undani wa maneno haya basi endelea-part-3




SHAIRI LA MCHA MUNGU-PART-3

Asalaam Aleiykum,

Jaribu kujikumbusha mfano huu wa kugundua au kupata(Uamsho)unapokua mzima wa afya hushughuliki na mguu wala mkono, hupati tabu ya kukumbuka meno wala masikio lakini wacha kimoja katika viungo hivo vipate maradhi utaona hapo (Attention)yote Akili yote inahamia hapo, deko lote linakuwepo hapo kwenye huo mguu, umeshapata kujiuliza kwanini? tega jicho uzuri tupo katika kuuchambua Moyo tupate siri zake ili tujue vipi tuna(Falling in  love)vipi tunapata hisia, inakuaje mahusiano haya na hii jinsi yangu mimi mwanaadamu, nini habari ya kipande hichi changu cha nyama kilichopo kwenye kifua changu.
Mcha Mungu kagundua Moyo ni chombo cha mawasiliano ya njia ya (Communion)inapata mawasiliano yake (Direct)au(Pure)mawasiliano haya iwe yanatokea huko kusikojulikana au hapa Ulimwenguni, yawe ya siri au dhahiri chombo hichi kina uweza wa kuya hifadhi iwe kwa kuona au kusikia.Ndio utaona Bwana Mtume s.a.w akaambiwa katika sura ya (Najm)"مَا كَذَبَ ٱلۡفُؤَادُ مَا رَأَىٰٓ""Moyo haukusema uongo (Kwa)uliyoyaona".
Kwani na wewe kuna mengi unayaona huwezi kuyakataa, hebu tizama Mfano huu wa mtoto mdogo, Analia, Anacheka ana hamaki na Akili yake bado haijakua, vitu hivyo vimetokea wapi, hakuna pengine isipokua Moyoni, hapo ndipo panapo kaa mapenzi, hisia, chuki, hamaki,furaha na imani na chochote kile kilicho husiana na hiyo (Communion)ndio maana utaona mfano huu kama una mgonjwa una uguza umekaa naye siku zote anapo kufa wewe wa karibu huzuni zako haziwi sawa na yule aliye mbali, kwa aliye mbali akiwasili anakua na huzuni kubwa sababu ya hiyo (Communion)ndio maana walimwengu wakasema unacho kitia moyoni taabu kukitoa, ndio Mcha Mungu akasema "nilipogundua katika huu Moyo wangu kumbe anaweza kukaa asiye kuwa wewe" mkapewa mfano katika Quraan vipi kitu kinaweza kuingia kikenda kukaa moyoni ili iwe alama kwenu.Quraan Aaraf-204,
" وَإِذَا قُرِئَ ٱلۡقُرۡءَانُ فَٱسۡتَمِعُواْ لَهُ ۥ وَأَنصِتُواْ لَعَلَّكُمۡ تُرۡحَمُونَ"
"Na Ikisomwa Quraan isikilizeni, Nyamazeni ili mpate kurehemewa".  hapo yametajwa mambo mawili la kwanza kusikiliza na la pili kunyamaza,Isikilizeni ili ipate kuingia kwenye moyo, usizungumze kwani ukizungumza haitokaa moyoni ipe nafasi itulie, ulipoambiwa nyamaza sio kwenye Akili unaendelea kuzungumza utakosa faida ya huko Kurehemewa, na kusudio la kurehemewa hapo ni hilo la (Uamsho), hivo wewe hujawahi kutengeneza kitu, au unafanya mtihani, au umeulizwa swali hujui jawabu lake umekaa una fikiri halafu ghafla linakujia jawabu, limetokea wapi, "Nilipojua katika huu Moyo wangu anaweza kukaa asiye kuwa wewe"hiyo ndio maana ya sikizeni na nyamazeni kimya yakiingia maneno ya Quraan katika nyoyo zenu yaka kaa basi tena hugeuka Imani na huko ndiko kurehemewa kuna patikana kwa njia ya sauti.
Endelea-part-4